The House of Favourite Newspapers

Yanga Yaiacha Simba Pointi 20, Yaipiga Mwadui 3-1

Kikosi cha Yanga kilichoanza dhidi ya Mwadui FC

KAMA unasubiri Yanga wapoteze mchezo msimu huu, hakika utasubiri sana. Hilo limeendelea kujidhihirisha jana wakati vijana hao wa Jangwani walipofanikiwa kuichapa Mwadui mabao 3-1 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kuendelea kuongoza Ligi Kuu Tanzania Bara.

 

Baada ya Simba kushinda kwa mabao 3-0 dhidi ya JS Saoura ya Algeria kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika, pia timu yao ya Simba Queens kuichapa Yanga Princess kwenye mchezo wa Serengeti Lite Women’s Premier League, walikuwa wanachonga sana, lakini dozi hii ya Yanga inawafunga mdomo.

Wachezaji wa timu ya Yanga.

Kuanzia msimu unaanza Yanga chini ya Mwinyi Zahera ilikuwa ikishinda, wengi wakasema kuwa hawana fedha wataanguka tu, lakini sasa wameonyesha kuwa wanawaacha Simba wanachonga, wao wanapiga kazi.

Katika mchezo wa jana, Ibrahim Ajibu aliendelea kuwa bora na kama hatapewa tuzo mwishoni mwa msimu basi itakuwa bahati mbaya.

 

Ajibu ambaye alijiunga na Yanga akitokea Simba msimu uliopita jana alionyesha kuwa msimu huu hazuiliki baada ya kuifungia timu yake bao safi la mkwaju wa faulo umbali wa mita 35 dakika ya 12 tu ya mchezo.

Kikosi cha timu ya Mwadui kichoanza dhidi ya Yanga.

Hili ni bao la sita kwa Ajibu msimu huu, akiwa nyuma kwa bao moja dhidi ya Meddie Kagere na Emmanuel Okwi wa Simba wenye mabao saba kila mmoja.

 

Hata hivyo, dakika nne tu mbele mtoto huyo wa Ilala alishindwa kuifunga timu yake bao la pili baada ya Amissi Tambwe kuchezewa madhambi na Ajibu kupiga penalti iliyopanguliwa na kipa wa Mwadui.

Pamoja na hivyo, bado Yanga waliendelea kuonyesha uwezo wao baada ya Tambwe kuifungia timu yake bao la pili dakika ya 38 kwa kichwa safi, huku akipata pasi toka kwa Ajibu. Hili ni bao la sita msimu huu kwa Tambwe kwenye ligi.

Ibrahim Ajibu akifanya yake Uwanjani.

Ajibu alifanya kazi nyingine nzuri katika dakika ya 58 baada ya kumpa pasi safi Fei Toto aliyefunga bao la tatu kwa timu yake akiwa nje ya 18.

Hii ni asisti ya 15 kwa Ajibu msimu huu na hakuna anayemsogelea.

Mshambuliaji wa Yanga Amissi Tambwe (kulia) akipongezana na Abdallah Shaibu ‘Ninja’.

 

Kwa sasa Yanga wamefikisha pointi 53 zikiwa ni 13 nyuma ya Azam waliopo nafasi ya pili na 20 nyuma ya Simba, ingawa Yanga wamecheza michezo mitano zaidi.

Dakika ya 82 Mwadui walipata bao la kufutia machozi lililofungwa na Salim Aiyee na kufanya dakika 90 kukamilika kwa Yanga kushinda mabao 3-1 dhidi ya Mwadui.

Said Ally na Ibrahim Musa/ PICHA: MUSA MATEJA

Comments are closed.