The House of Favourite Newspapers

Yanga Yaipiga Simba Bao Kwa Denis Kibu

0

 

 

YANGA imefikia muafaka mzuri na Mbeya City katika kufanikisha usajili wa mshambuliaji Denis Kibu huku tetesi zikisema kuwa nyota huyo atajiunga na klabu hiyo kwa mkataba wa miaka minne wenye thamani ya Sh 150Mil.

 

Hiyo ni baada ya pande zote za Yanga na Mbeya City kukubaliana katika dau hilo ili wamuachie nyota huyo kujiunga na mabingwa wa kihistoria nchini.

 

Awali mshambuliaji huyo ilielezwa kuwaniwa na Simba akiwa kwenye kambi ya Taifa Stars iliyokuwa inajiandaa na mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Malawi uliochezwa wikiendi iliyopita kwenye Uwanja wa Mkapa.

 

Mmoja wa mabosi wakubwa wenye ushawishi wa usajili ndani ya Yanga, ameliambia Championi Jumatano kuwa, klabu hizo mbili zimefikia muafaka mzuri huku Mbeya City ikikubali kumuachia baada ya mchezaji mwenyewe kuomba aachiwe ili ajiunge na timu hiyo.

 

Bosi huyo alisema kuwa dili hilo la usajili tayari limekamilika tangu juzi na kinachosubiriwa ni mchezaji kusaini mkataba huo mnono wa miaka minne wa kuichezea Yanga wenye thamani hiyo kubwa ya fedha ambazo nyingine zitakwenda kwenye klabu yake.

 

“Klabu yake ya Mbeya City imekubali kiroho safi kumuachia Kibu kujiunga na Yanga ni baada ya viongozi wa pande hizo kukutana na kufikia muafaka mzuri wa mchezaji huyo kusaini Yanga baada ya majadiliano ya muda mfupi.

 

Kibu mwenyewe ameonyesha nia ya kuja kuichezea Yanga badala ya Simba akiamini ni sehemu yake sahihi ya kuja kuichezea katika msimu ujao.

 

“Hivyo Kibu atasaini mkataba wa miaka minne wenye thamani ya Sh 150 Mil kwa ajili ya kuichezea Yanga,” alisema bosi huyo ambaye hakutaka jina lake liweke wazi.

 

Mbeya City kwa kupitia katibu wake, Emmanuel Kimbe, alithibitisha kuwepo mazungumzo ya mwisho ya kufanikisha usajili wa mshambuliaji huyo.“Ni kweli mazungumzo yamefikia pazuri na Yanga na huenda Kibu akajiunga na timu hiyo katika msimu ujao baada ya timu hiyo kukubali kutoa dau la usajili ambalo sisi tunalitaka ili tumuachie aende huko.”

 

Kwa upande wa Yanga, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa timu hiyo, Hassani Bumbuli alisema kuwa: “Tunasubiria ripoti ya kocha wetu na baada ya hapo kila kitu kinachohusiana na usajili tutakiweka wazi, kingine muda wa usajili bado uongozi upo kwenye maandalizi kwa ajili ya michezo yetu ya ligi ukiwemo dhidi ya Ruvu Shooting.”

STORI: WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Leave A Reply