Yanga Yaisaidia Namungo Kimataifa
KOCHA mkuu wa Namungo, Hemed Morroco amesema kuwa sare waliyoipata dhidi ya Yanga ni maandalizi tosha kuelekea katika mchezo wa Kimataifa dhidi ya Al Rabita FC ya Sudan Kusini.
Namungo ambao wanashiriki michuano ya Kombe la Shirikisho wanatarajia kuwa wenyeji wa Al Rabita katika mchezo unaotarajia kufanyika wikiendi hii katika Uwanja wa Azam Complex jijini Dar.
Akizungumza na Championi Jumatano, kocha huyo alisema kuwa ukiachana na matokeo ya sare waliyoyapata dhidi ya Yanga, kucheza dhidi ya timu hiyo kwao yanakuwa maandalizi mazuri kuelekea kwenye mchezo wa kwanza wa michuano hiyo.
“Yanga ni timu ya hadhi ya michuano ya kimataifa na hivyo ukiachana na matokeo ambayo tuliyapata ya sare ya bao 1-1, tunachokiangalia zaidi ni maandalizi kuelekea mchezo wetu.
“Hakika Yanga imetupa changamoto nzuri ambayo naamini itatusaidia kuelekea katika mchezo wetu ujao wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Al Rabita FC,” alisema Morocco.
Marco Mzumbe, Dar es Salaam