VINARA wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga tayari wametinga ndani ya Jiji la Mbeya kuwakabili Wajelajela Tanzania Prisons, leo Jumatatu.
Yanga ambayo ilitumia usafiri wa ndege kutua jijini hapa, imekuwa na matokeo mazuri kwenye michezo yao ya hivi karibuni.
Mjumbe wa Kamati ya Mashindano ya Yanga ambaye pia ndiye aliyeongoza mapokezi ya timu hiyo kwenye Uwanja wa Ndege wa Songwe, Kayanda Sanga amewataka mashabiki na wanachama wa timu hiyo kujitokeza kwa wingi kuipasapoti timu yao.
“Tunamshukuru Mungu tumefanikiwa kuipokea timu salama na kilichobaki ni kupambana kuhakikisha timu inapata ushindi dhidi ya Prisons,” alisema.
Kabla ya kukutana leo kwenye Uwanja wa Sokoine, ikumbukwe kuwa katika mchezo wa mwisho ambao ulizikutanisha timu hizo katika ligi msimu uliyopita, Yanga ilikubali kipigo cha mabao mawili.
Kocha wa Prisons, Mohammed Abdallah, amesema kuwa wamejipanga kuhakikisha wanapata matokeo.
“Tumejipanga kuhakikisha tunapata matokeo mazuri dhidi ya Yanga kwenye mchezo huu, hivyo mashabiki wajitokeze kwa wingi,” alisema Abdallah.
DERICK LWASYE, Mbeya
Comments are closed.