The House of Favourite Newspapers

Yanga Yampigia Simu Kocha Mpya

0

TAKRIBANI siku tatu sasa, Yanga imekuwa kwenye kikao kizito cha kupitisha jina moja la atakayekuja kuwa kocha mkuu wa klabu hiyo, ambapo tayari mabosi na kamati tendaji yake ilimfanyia mahojiano kocha wa zamani wa Township Rollers, ya Botswana, Nikola Kavazovic, raia wa Serbia ili aje kuziba pengo la Cedrick Kaze aliyetimuliwa mwishoni mwa wiki iliyopita kabla ya mechi yao na Simba kufika.

 

Yanga wanaonekana dhahiri kuridhishwa na utendaji kazi wa Mserbia Kavazovic, kwani alipokuwa akiinoa timu ya Township Rollers, kabla ya kuachana nayo Novemba mosi msimu wa 20/21, msimu wa 2017-18, alifanikiwa kuchukua ubingwa wa ligi hiyo na kuifanikisha kucheza Ligi ya Mabingwa Afrika kisha kutimkia katika timu ya Leopards ya Kenya.

 

Mbali na hivyo pia Kavazovic aliifundisha Free State Stars ya Afrika Kusini kwa msimu mzima na baadaye kuachana nayo na kubaki akifanya mambo yake binafsi jambo linalowapa Yanga unafuu wa malipo kiasi cha kumtaka aje kuungana na Juma Mwambusi ambaye hadi sasa ndiye aliyetajwa kuendelea na kikosi hicho.

 

Chanzo chetu kimeliambia Championi Ijumaa kuwa, tangu uongozi wa Yanga, utangaze kuachana na Kaze, umekuwa ukiketi mara kwa mara ili kuhakikisha wanampata mrithi wake kabla ya mwezi huu kuisha, ambapo tayari wamefanya naye mahojiano ya mwisho kwa njia ya simu na kikao cha uamuzi kimepeleka jina kwa mdhamini wao Kampuni ya GSM ili iweze kukubaliana naye malipo yake.

“Kimsingi kocha anayeonekana kutuvutia sana hadi muda huu ni yule kocha wa zamani wa Township Rollers na kwamba kamati zote zimekaa na zimeamua kutohangaika sana kwani lengo ni kumpata kocha mapema kabla ya mchezo wetu wa Mei na Simba haujafika, hivyo plani zetu ni kumpata kocha ndani ya mwezi huu wa tatu.

 

“Hadi muda huu kocha anayeonekana kwenye vikao vya kamati tendaji na uongozi ni huyu Mserbia, ambapo kwenye vikao vyote vya siku mbili kwa maana na leo na jana (Jumatano na Alhamisi) wamejiridhisha naye kiasi kwamba tayari wamempigia simu na kufanya naye mahojiano kisha wamefikisha jina kwa wadhamini wetu ili nao wajiridhishe na kupanga dau lake.

 

“Tumelazimika kufanya haraka suala la kumpata kocha ndani ya mwezi huu awe ameshatua nchini ili aje kuzoeana na wachezaji kabla ya mchezo wetu na watani wa jadi kuwadia ambapo ukiangalia tuna muda mchache sana kuufikia huo mwezi wa tano,” kilisema chanzo hicho.

Ikumbukwe Simba na Yanga zimepangwa kukutana Mei 8, mwaka huu katika mchezo wa Ligi Kuu Bara.

STORI; MUSA MATEJA, Dar es Salaam

Leave A Reply