The House of Favourite Newspapers

Yanga yashusha straika Mtogo

0

MAMBO sasa kimyakimya tu kwani Yanga ipo mbioni kumleta straika hatari kutoka Togo ambaye ataingia moja kwa moja katika kikosi cha kwanza akiwa maalum kwa mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika.

Straika huyo anatarajiwa kutua nchini siku yoyote kuanzia sasa kabla ya dirisha la usajili kufungwa, Desemba 15, mwaka huu ili kumalizana na uongozi wa timu hiyo.

Habari za kuaminika kutoka ndani ya Yanga zimedai kuwa, uamuzi wa kumleta mchezaji huyo umefikiwa hivi karibuni na benchi la ufundi linalotaka kuwa na kikosi hatari kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika iliyo chini ya Shirikisho la Soka Afrika.

“Uongozi unafanya siri kubwa, yaani hautaki kabisa watu wajue juu ya hili kwani unahofia dili hilo linaweza kuingiliwa kati na wapinzani wao.

“Lakini ukweli ni kwamba, straika huyo atatua hapa nchini siku yoyote kabla ya dirisha la usajili kufungwa ili aweze kumalizana na uongozi na jinsi inavyoonekana wanataka kufanya mambo kimyakimya.

“Endapo straika huyo atamalizana na uongozi, kuna uwezekano mkubwa Vincent Bossou akafungashiwa virago kwa sababu kiwango chake ni cha kawaida sana na tayari mipango ya kumalizana naye imeshaanza,” kilisema chanzo hicho.

Katibu Mkuu wa Yanga, Dk Jonas Tiboroha, alipotafutwa ili kuzungumzia taarifa hizo, hakuweza kupatikana kwani simu yake iliita bila kupokelewa.

Akiwa katika mipango ya usajili hivi karibuni, Kocha wa Yanga, Hans van Der Pluijm, aliliambia gazeti hili kuwa, watafanya usajili wa siri kwa mchezaji aliyekamilika ili wawe na kikosi bora kwa mechi za Afrika.

Leave A Reply