Yassin Atibua Mambo Yanga
BAADA ya kuwa nje ya uwanja akiuguza majeraha ya muda mrefu, beki wa kushoto wa Yanga, Yassin Mustapha amepona na kurejea kikosini huku akiibua vita mpya ya namba katika nafasi hiyo.
Wachezaji waliopo katika nafasi hiyo ni David Bryson, Adeyum Saleh, Kibwana Shomari na Yassin ambaye msimu uliopita kabla ya kuumia alikuwa kikosi cha kwanza.
Wakati Yassin akiuguza majeraha, kocha wa timu hiyo, Nasreddine Nabi aliamua kumhamisha nafasi Kibwana kutoka beki wa kulia na kucheza beki wa kushoto ambapo sasa kurejea kwa Yassin kunampa machaguo mengi zaidi Kocha Nabi kupanga kikosi chake.
Kwa mujibu wa chanzo cha ndani kutoka ilipo Kambi ya Yanga maeneo ya Avic Town, Kigamboni, Dar, kimeliambia Spoti Xtra kuwa: “Yassin Mustapha amerejea kikosini baada ya majeraha ya muda mrefu na tayari ameanza mazoezi mepesi na wenzake.
“Alianza mazoezi Jumatano ambapo kocha wa utimamu wa mwili amesema anahitaji siku 30 ili kuwa fiti zaidi na kuanza kucheza mechi.”
LEEN ESSAU, Dar