The House of Favourite Newspapers

Yondani Atii Amri

BEKI Mkongwe wa Klabu ya Yanga, Kelvin Yondani amesema kuwa anakubali uwezo wa beki mwenzake raia wa Ghana, Lamine Moro na kwamba uelewano wao umefanya wawe na safu bora ya ulinzi kwa kipindi hiki.

Moro alijiunga na Yanga wakati wa dirisha la usajili na tayari ameshakuwa beki tegemeo ndani ya Yanga kutokana na kazi kubwa aliyoifanya katika michezo kadhaa aliyoitumikia klabu hiyo hasa katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Township Rollers.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Yondani alisema Moro amekuja kuongeza kitu katika safu yao ya ulinzi kwa kuwa kipindi hiki kifupi tayari ameonyesha utofauti na umuhimu wake katika nafasi ya ulinzi na kwa hali ilivyo msimu huu utakuwa bora zaidi kwao kutokana na ukali wao katika kuzuia mashambulizi.

“Lamine ni beki mzuri sana, kwa sababu katika kipindi hiki kifupi tayari ameshaonyesha ubora wake katika kuzuia mashambulizi, kila mmoja ameona namna ambavyo anacheza kwa umakini akiwa katika eneo lake.

“Msimu uliopita tulikuwa na safu nzuri ya ulinzi, lakini msimu huu naona imeongezeka zaidi kwa kuanzia mabeki wa pembeni na kati, hiyo ni kutokana na usajili bora uliofanywa na viongozi. Ni matarajio yangu kuona msimu huu tukifanya vizuri katika ligi na michuano ya kimataifa,” alisema Yondani.

ISSA LIPONDA, Dar es Salaam

Comments are closed.