Zahera amkwepa Mo Dewji
KOCHA Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera, amepiga hesabu za mbali na kuamua kufanya usajili wake mapema kwa ajili ya kuwakwepa vigogo wa kamati ya usajili ya Simba ambao wanaongozwa na mwekezaji bilionea Mohammed Dewji ‘Mo’.
Kocha huyo ameamua kuja na mbinu ya kusajili wachezaji anaowataka mapema kabisa kabla ya ligi kumalizika sambamba na kuwapa mikataba wachezaji anaowahitaji ili kukwepa kugombania saini za wachezaji kwenye kipindi cha usajili.
Mmoja wa wajumbe wa kamati ya Yanga ameliambia Championi Jumatatu kuwa Zahera amefanya mbinu hiyo ili itakapofika wakati wa usajili, yeye awe bize kukinoa kikosi chake kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu. “Kuna fungu ambalo kocha ametengewa kwenye hizi fedha za michango kwa ajili ya kusajili wachezaji ambao anawataka lakini bado wanafanywa siri.
“Wazo la kocha ni kusajili mapema kwani wakati wa dirisha la usajili anataka kutuliza timu iwe inafanya mazoezi ili wachezaji wapya na wale wa zamani waweze kuzoeana kwa haraka, lakini pia kutokuwa na vita ile ya kugombea wachezaji na timu nyingine.
“Anachotaka ni kuona timu inakuwa na muunganiko mzuri msimu ujao, ndiyo maana ametoa kile anachotaka ili afanyiwe mapema,” kilisema chanzo hicho. Zahera mwenyewe amesema kuwa kwa msimu ujao anachokitaka ni kukifanyia marekebisho kikosi hicho japo hadi sasa bado hajajua ni wachezaji gani ambao ataachana nao.
Akizungumza na Championi Jumatatu jana mchana, Zahera alikubali kuwa watafanya usajili wa mapema zaidi. “Ni kweli, lakini kikubwa kwa sasa tunachosubiri ni suala la fedha, kama fedha ikipatikana basi tutafanya usajili wetu mapema,” alisema Zahera.
Baadhi ya wachezaji ambao Yanga imeripotiwa kuwataka ni straika Jacque Tuyisenge raia wa Rwanda anayeichezea Gor Mahia na Yannick Bangala Litombo ambaye ni beki wa kati wa AS Vita ya DR Congo.
WAFUNGAJI
Comments are closed.