Zahera: Makambo Habari Nyingine, Atafunga Sana Tu
KOCHA Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera raia wa DR Congo ameweka wazi kwamba anamuamini straika wake, Heritier Makambo kuwa ana uwezo wa kufunga zaidi ya mabao 16 kwenye ligi kutokana na kufunga idadi hiyo kwenye ligi ngumu ya Congo.
Makambo ana mabao saba sambamba na washambuliaji wa Simba, Meddie Kagere na Emmanuel Okwi .
Akizungumza na Championi Ijumaa, Zahera amesema kwamba anamuamini kwa sababu tayari alishafanya naye kazi nchini Congo na alifunga mabao mengi akipambana na timu kama TP Mazembe, hivyo hawezi kushindwa kufunga katika ligi ya Tanzania kutokana na kutokuwepo ugumu sana kulinganisha na huko.
“Wakati ambao Makambo hakuwa anafunga mashabiki wakaanza kuongea lakini niwaambie kwamba hilo suala siyo ishu kwake kwa sababu nimefanya naye kazi DR Congo aliwahi kufunga mabao 16 kwenye mechi nane za ligi.
“Kwenye suala la kufunga ninamuamini kwamba hataniangusha na niwaambie kwamba atafunga zaidi, ni suala la kupewa muda tu,” alisema Zahera.
Stori na Said Ally,
Comments are closed.