The House of Favourite Newspapers

Zitto Kabwe Amtaka Rais Magufuli Avunje Bunge

Mbunge wa Kigoma Mjini Zitto Kabwe amemshauri Rais wa Tanzania Dkt. John Magufuli kulivunja Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania endapo analiona ni kikwazo kwake.
Ushauri huo ameutoa jana ikiwa ni saa chache baada ya Rais Magufuli kukosoa uamuzi wa Bunge kumuita Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda kujieleza mbele ya Kamati ya Bunge, kutokana na kilichodaiwa na wabunge kuwa ni kauli ya kulidhalilisha Bunge.
Katika hotuba yake aliyoitoa jana wakati wa kuapishwa kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Rais Magufuli aliwataka viongozi wengine kumuunga mkono mtu anayejitokeza kupiga vita dawa za kulevya badala ya kumdhalilisha.
“Tunapomuona mtu anajitokeza kupambana na haya madawa ya kulevya, badala ya kumdhalilisha tumuombee na kumtia moyo, hawa wanaweza hata kubadilisha maneno uliyoyazungumza wakabadilisha wakatengeneza kwenye clip wakatupa, na wakajitokeza wengine wakasema wameingilia mamlaka yao, wakati wao wanaingilia mamlaka ya kuwaita wengine, hii ni vita”. Alisema Magufuli
Baada ya kauli hiyo ya Rais, Zitto kupitia ukurasa wake wa Facebook ameonesha kushangazwa na kile alichodai  kuwa Rais hakujua kuwa sheria ya kuundwa kwa mamlaka hiyo, ilitungwa, na kwamba anashangaa kuona Rais hakuwa akijua kuwa alipaswa kumteua Kamishna Mkuu wa Mamlaka hiyo
Ujumbe wa Zitto unasema
“Wabunge walitoa Hoja Binafsi kuhusu Madawa ya kulevya ( Esther Bulaya na Faustine Ndugulile ) na kufuatia hoja hiyo Serikali ikaleta Muswada bungeni na Bunge likatunga Sheria ya Kupambana na Madawa ya kulevya mwaka 2015.
 
“Serikali mpya ikaingia madarakani mwezi Novemba 2015. February 2017 Ndio Kamishna Mkuu anateuliwa tena baada ya wabunge kuhoji na kushinikiza kupitia Kamati husika na pia mbunge Esther Bulaya aliyetoa Hoja Binafsi katika Bunge la Kumi.
“Rais anasema hakuwa anajua kuwa sheria hiyo ipo. Lakini Rais anapogawa Wizara huwa anatoa instruments na Hizo instruments hutaja kila sheria kwa kila Waziri. Ilikuwaje Rais akasahau sheria hii nyeti kama alikuwa na nia ya dhati ya Kupambana na Madawa ya kulevya?
 
Rais anaona Bunge kikwazo kwa sababu Bunge linamwongoza afuate sheria. Lakini Kama anaona Bunge linamkera turudi kwenye uchaguzi tu, alivunje”.

Comments are closed.