ZOEZI lililopangwa kufanyika leo Agosti 1, 2020, la aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar, Paul Makonda, kukabidhi rasmi ofisi kwa mkuu mpya wa mkoa huo, Aboubakar Kunenge, limesogezwa mbele hadi Jumatatu Agosti 3, 2020, kufuatia Kunenge kubanwa na majukumu ya ufunguzi wa maonyesho ya Nanenane.
Taarifa ya kuahirishwa kwa zoezi hilo imetolewa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, ambapo hii leo Agosti Mosi, Makonda alitarajiwa kukabidhi ofisi hiyo iliyopo maeneo ya Ilala, majira ya saa 7:00 mchana.
Makonda aliondolewa kwenye nafasi hiyo siku ya Julai 15, 2020, na Rais John Pombe Magufuli, baada ya kuchukua fomu ya kuwania kuteuliwa kugombea ubunge wa Kigamboni (CCM), na nafasi hiyo ilichukuliwa na aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa huo.
Machi 13, 2016, Magufuli alimteua Makonda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, ambapo awali kabla ya uteuzi huo alikuwa ni Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni na hivyo amehudumu kwenye nafasi ya ukuu wa mkoa kwa zaidi ya miaka mitatu.