The House of Favourite Newspapers

Dereva achinjwa kikatili

IMG-20151120-WA0003Salum Masoud enzi za uhai wake.

 

Na Boniphace Ngumije
INASIKITISHA! Salum Masoud (35), mkazi wa Kijichi, Rufiji mkoani Pwani ambaye alikuwa dereva wa magari ya kubeba mizigo mkoani humo ameuawa kikatili kwa kuchinjwa na watu wasiojulikana na ifuatayo ni simulizi ya kusikitisha kutoka kwa dada wa marehemu aitwaye Hawa Masoud, mkazi wa Mbagala, Dar.

Akifuta machozi na kuzungumza kwa kwikwi na gazeti hili hivi karibuni, Hawa alisema mazingira ya tukio la kuchinjwa kwa ndugu yake yamejaa utata.

“Taarifa za kuuawa kwa kaka yetu zilitufikia Novemba 10, mwaka huu baada ya watu wasiojulikana kumpigia simu dada wa mke wa marehemu na kumtaarifu.

IMG-20151120-WA0013“Binafsi nilishtushwa sana. Ilikuwa vigumu kuamini. Lakini hatukuwa na budi kukubaliana na hali halisi, tukaamua kukusanyana na kwenda eneo la tukio kufahamu nini kilitokea mpaka Salum akauawa kikatili namna hiyo.

“Tulipofika tulimkuta bosi wa marehemu aitwaye, Salum Bakari Mnolage akifanya taratibu za mazishi. Tulimkataza lakini akatuitia mashehe kutuambia taratibu za Dini ya Kiislamu juu ya kufanya mazishi mapema baada ya kifo.

“Hatukukubali, tukaenda kituo cha polisi kilicho karibu ili kupata haki ya kumchukua marehemu, lakini tukiwa katika harakati hizo, mwili wa marehemu ulizikwa na tulipohoji tuliambiwa kama haturidhiki na hatua hiyo tukaufukue. Lakini hatukufanya hivyo na tumemwachia Mungu.”

Gazeti hili lilimtafuta mpelelezi wa kesi ya ndugu hao kutaka kupewa haki ya kuuchukua mwili wa ndugu yao, yeye alisema:

“Ni kweli tukio hilo lipo na kama unavyofahamu kesi hizi zinakuwa na mambo mengi. Kwa sasa bado tunachunguza, tukikamilisha taratibu, sheria itafuatwa.”
Marehemu ameacha mjane Sikujua Iddi na watoto watatu. Mwili wake ulizikwa Kijiji cha Kijichi, Rufiji, Pwani.

Comments are closed.