The House of Favourite Newspapers

Kwa Heri Ndanda Kosovo ‘Kichaa’

1

 

12934847_1064063696984266_1609999490_n

Mwanamuziki mwenye asili ya Demokrasia ya Kongo Ndanda Kosovo enzi za uhai wake.

Makala: Boniphace Ngumije

KWA vijana waliokua miaka ya 2000, wapenzi wa Muziki wa Dansi, jina la Ndandason Onawembo ‘Ndanda Kosovo’, mwenye asili ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), halitakuwa geni.

Ndanda alianza safari yake ya muziki akiwa nyumbani kwao Kongo ambapo baada ya kutua nchini alitamba na Bendi ya FM Academia International iliyokuwa maarufu baada ya kutoa Wimbo wa Wajelajela.

Katika wimbo huo Ndanda alishirikiana na wasanii wakali ambao ni pamoja na Nyoshi El-Sadaat, Maluu Stonch, Mulemule FBI, King Blaize, Patcho Mwamba, Gento na wengine wengi waliuimba baada ya kutoka jela walikokuwa wameshikiliwa kwa ishu za kutokuwa na vibali vya kuwaruhusu kuishi  na kufanya kazi Bongo.

Baadaye Ndanda aliachana na Bendi ya FM Academia baada ya kuanzisha bendi iitwayo Stono Musica au Wajelejela Original akiwa na Maluu, Chai Jaba, Patcho na wengineo. Miongoni mwa nyimbo walizotamba nazo wakiwa na bendi hiyo ni pamoja na Binadamu, Kaokota Big G na Kidedea.

Hata hivyo, Ndanda hakudumu sana na bendi hiyo baadaye alitimkia Marekani kwa shughuli za kimuziki, aliporejea Bongo alijikita mkoani Arusha na kuanzisha Kundi la Watoto wa Tembo kabla ya kuachana na bendi na vikundi na kuwa msanii anayejitegemea.

ndanda-2

Akifanya yake enzi za uhai wake.

Kabla ya kukutwa na umauti, historia ya ugonjwa wake inaonesha alianza kusumbuliwa mwaka jana na tatizo la kupasuka kwa mmoja ya mishipa tumboni hivyo kutapika damu lakini madaktari walijitahidi akapona na kuendelea na shughuli zake.

Ndanda alianza kuugua tena hivi karibuni akisumbuliwa na tumbo ambapo alilazwa kwenye Hospitali ya Mwananyamala na baadaye kuhamishiwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar, mauti yalipomkuta majira ya asubuhi leo hii.

Baadhi ya mafanikio aliyoyapata kwenye kazi yake ya muziki  ni pamoja na kukubalika na kufahamika na watu wengi nchini, kumudu kuendesha maisha yake mwenyewe pamoja na familia.

MUNGU AILAZE ROHO YAKE MAHALI PEMA PEPONI, AMINA.

 

1 Comment
  1. Epafras says

    Namiumia nilikuwa shabiki Wake, kwanza kwa uwezo wake wa kuimba pili jamaa ana fanana sana na brother wangu nilikuwa nikimuona naenjoy kwanza kwa uimbaji wake pili namkumbuka Kaka yangu, Rest In Peace brother I will remember you all the time through your music.

Leave A Reply