The House of Favourite Newspapers

‘Userious’ sana unaharibu ladha ya mapenzi

0

ladha ya mapenzi

MAPENZI yana raha kama pande mbili zikiwa na amani. Mwanamke awe na amani, mwanaume pia. Tofauti na hapo, penzi hugeuka mateso kwa mmoja wapo. Uhusiano unapoteza mvuto, mtaishia kuachana. Mapenzi yanapendeza wawili mkifanana.

 

Mkiendana kitabia, kifikra. Mtainjoi zaidi uhusiano kama mkiwa mnazungumza lugha moja na mwezi wako. Mnakwenda sawa katika kila jambo. Kwenye wakati wa furaha, mnakuwa pamoja na kwenye huzuni hali kadhalika. Mapenzi yanahitaji lugha rafiki. Wakati mwingine yanahitaji kuchombezana, kuliwazana na kama haitoshi kudekezana.

 

Kuna wakati mwenzako anaweza kufanya jambo unaloweza kuliona ni la ‘kijinga’, kakutania, yote hiyo ni mapenzi tu. Anahitaji kukuona unacheka. Anapenda kukuona una furaha wakati wote. Anakutania anakusemesha hata mambo ambayo wakati mwingine unaweza kuona hayana maana. Anakuuliza vitu ambavyo havina kichwa wala miguu.

 

Katika hili wanaume wengi ni waathirika. Ukizungumza na wanaume wengi watakupa ushuhuda wa aina hii; ‘wanawake bwana sijui wapoje? Wakati mwingine wanakuwa na mazunguzo yasiyo na msingi. Wanaboa kweli wakati mwingine’ Mathalan, anauliza swali ambalo jibu lake analo. Anataka tu umjibu. Si kwamba hafahamu jibu lake, anajisikia tu furaha ukimjibu wewe mpenzi wake.

 

Akiwa na wewe anataka mcheke. Anatamani umdekeze, moyo wake unasuuzika. Kutokana na pilikapilika za kila siku za maisha au kutokana na hulka za baadhi ya watu, wapo baadhi ya watu ambao kwa namna moja au nyingine suala la kuwa ‘romantic’ linawashinda. Yeye wakati wote yupo serious. Humuoni akicheka. Muda wote sura yake ni ya kazi.

 

Hana mazungumzo ya utani hata kidogo. Sura anayokuwa nayo anapokuwa na rafiki zake wenye jinsia yake, ndiyo hiyohiyo anaiweka anapokuwa na mpenzi wake. Anaishi ‘kikakamavu’ kama vile askari. Akiwa kazini, akiwa mtaani na wenzake, akiwa chumbani lugha yake ni moja.

 

Anaongea kwa ukali. Hakuna muda wa kuchekacheka. Yeye ni mtu wa amri tu na kusubiri utekelezaji. Amri anazozitoa kwa wafanyakazi wenzake ofisini ndizo hizohizo anazitoa kwa mkewe. Kila muda yupo serious, ni mtu wa kutoa maagizo. Neno lake ni kama sheria. Inafika mahali hata watoto wanamuogopa.

 

NI TATIZO

Unapokuwa kwenye uhusiano halafu muda wote unakuwa serious, inaondoa uzuri wa uhusiano. Unatengeneza mipaka kati yako na mwenzi wako.

 

HUPUNGUZA URAFIKI

Ukiwa serious sana, mwenzi wako anapunguza urafiki. Anakuhofia, matokeo yake analazimika kuzungumza utani na mtu mwingine ambaye anapenda utani kwelikweli.

 

HUONGEZA USHAWISHI WA USALITI

Iko wazi, mwenzi wako anapokosa raha ya uhusiano kwako, akiwa na moyo mdhaifu anaweza kushawishika kusaliti endapo tu atakutana na mtu atakayempa kile ambacho wewe humpi.

 

KUWENI ROMANTIC

Mwanaume unapaswa kuwa mlaini kidogo kwa mwanamke vivyo hivyo mwanamke. Kweli kuna wakati mkubwa zaidi wa kuutumia mkiwa serious lakini msisahau kuwa na utani, kuchekeshana kwa hapa na pale na mambo mengine kwani yanaongeza utamu au maana ya penzi.

 

VUMILIANENI

Wakati mwingine unaweza kuona kwamba utani au vitu vya mzaha anavyokueleza mwenzako havina maana lakini hakuna namna, msikilize na umuunge mkono. Mtaniane kwa kiasi, mcheke kwa kiasi kwani ndiyo chachu ya kuufanya uhusiano wenu uwe hai. Mkizingatia hayo, mtaishi vizuri na mtafurahia uhusiano.

 

NA: ERICK EVARIST +255 768 811595

Leave A Reply