MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amewashauri wanafunzi wa mkoa wake kusoma masomo ya sayansi ili kuendana na teknolojia inayokua duniani.
Mwenyekiti wa bodi ya taasisi za shule za Al Muntazir, Imtiaz Laiji, akizungumza.
Hayo ameyasema leo wakati akikabidhiwa msaada wa madawati 200 yenye thamani ya Sh. milioni 20 na taasisi ya shule za Al Muntazir zilizopo Palm Beach jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa jumuiya wa shule hizo, Azim Dewji, akizungumza.
Akizungumza katika hafla hiyo, Makonda amesema wanafunzi wa mkoa wake wanapaswa kutilia mkazo katika kusoma masomo ya sayansi ili kuendana na soko linalozidi kukua katika maendeleo ya ajira kutokana na teknolojia katika sayansi.
…Makonda akikata utepe kuashiria kukabidhiwa msaada wa madawati hayo.
“Wanafunzi kwa kuhamasishwa na wazazi wenu mnapaswa kusoma masomo ya sayansi ili muweze kuendana na ajira zilizopo hivi sasa hasa ukiangalia sasa hivi tuna miundombinu ya mafuta na gesi inayohitaji wataalam wa sayansi na hata katika kukuza wigo wa viwanda hapa nchini,” alisema.
Alifafanua kuwa mwanafunzi atayefanikisha kufaulu vizuri katika masomo yake ya sayansi atapata msaada wa kusomeshwa hadi nje ya nchi, na mwalimu wake atakayekuwa amemwezesha kufaulu atapatiwa Sh. milioni mbili kama zawadi na kula raha katika mbuga za wanyama kwa muda wa siku mbili.
Makonda (wa pili kushoto) akiwa na viongozi wa shule.
Naye mwenyekiti wa bodi ya taasisi za shule za Al Muntazir, Imtiaz Laiji, alisema kutoa mchango wao huo wa madawati ni juhudi zao katika kuhakikisha serikali inasonga mbele kimaendeleo ya kielimu.
“Hivi karibuni shule za Al Muntazir ziliwadhamini walimu wakuu kumi kutoka shule za serikali za mkoa wa Dar es Salaam kushiriki mafunzo ya uongozi bora wa shule ili kuisaidia serikali katika kuwapatia mafunzo.
Baadhi ya wanafunzi wa shule ya Al Muntazir waliohudhuria hafla hiyo.
“Ingawa shule hizi zinamilikiwa na taasisi ya dini, udini na ubaguzi haupo katika shule hizi, wanafunzi wa madhehebu yote ya dini wanaruhusiwa kusoma katika shule zetu.
Makonda akisalimiana na wanafunzi wa shule hiyo.
“Walimu na wafanyakazi wake pia ni wa dini na madhehebu yote na huu ni mfano mzuri wa ushirikiano bila kujali dini kwa kuwa sote tumeumbwa na Mungu mmoja,” alisema.
…Akiendelea kubadilishana nao mawazo.
Mchango huo ni moja kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli katika kuwapatia mazingira bora ya kujifunzia wanafunzi.
Na Denis Mtima/Gpl.

