Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda akijaribu mojawapo ya mashine za kutengeneza barabara ya Kampuni ya Grand Tech.
DAR ES SALAAM: Kampuni ya Grand Tech ya nchini Tanzania imejitolea kujenga barabara ya Shimo la Udongo kwa kiwango cha zege kwa urefu wa Kilomita moja, ikiwa ni ishara ya kuunga mkono jitihada za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda na Rais Dk. John Pombe Magufuli.
Akizungumza Jijini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi wa Kampuni hiyo inayojihusisha na ujenzi wa barabara na makazi Atu Patrick Mwakitwange ameeleza kuwa wameamua kuunga mkono jitihada za serikali kwani eneo hilo la Shimo la Udongo lilitengwa na serikali kwa ajili ya shughuli za bandari hivyo ujenzi huo utarahisisha shughuli hizo na wataendelea kuunga mkono jitihada za Rais Magufuli.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda wakati akizindua ujenzi huo ameeleza kuwa Dar es Salaam inajengwa na wana Dar es Salaam wenyewe hivyo kila mmoja kwa mchango wake kusaidia kadri awezavyo kama walivyojitokeza wazawa na Grand Tech kujenga barabara hiyo huku akiongeza kuwa wazawa hao ndiyo wazawa wa kwanza kwa Mkoa wa Dar es Salaam kujenga barabara na kuwaomba wadau wengine waige mfano huo.
Vilevile RC Makonda ameeleza kuwa barabara hiyo inatija kubwa kwa serikali kwani ujenzi wake kwa kiwango cha zege utasaidia malori kupita bila kufanya uharibifu kama ilivyokuwa awali, pia ujenzi huo utasaidia kupunguza foleni.
Na Hilaly Daud / GPL




