Barcelona, Hispania
KLABU ya Barcelona imeonyesha kuwa hakuna mtu muhimu kwenye timu hiyo zaidi ya mshambuliaji wake Lionel Messi baada ya kumtimua mkurugenzi aliyemkosoa mchezaji huyo.
Mkurugenzi wa klabu hiyo Pere Gratacos, alimkosoa Messi kwenye mchezo wa Copa del Rey aliposema kuwa staa huyo asingeweza kufanya vizuri uwanjani kama wasingekuwepo Andres Iniesta na Neymar na wachezaji wengine.
Barcelona imekuwa ikimhusudu Messi kwani wachezaji wengi wamekuwa wakilalamika kuwa endapo utamzungumzia vibaya mchezaji huyo mwenye tuzo tano za Balon d’Or, utaondoka klabu hapo.
Mkurugenzi huyo alipoulizwa nafasi ya Messi kwenye mchezo huo uliopita dhidi ya Athletic Bilbao, mchezo ambao Messi alifunga kwa faulo na kuwapitisha Barcelona alisema: “Siyo Lionel Messi pekee, tunajua kuwa Leo ni kati ya wachezaji mahiri kwenye timu hii.
“Lakini Barcelona walifuzu kwenda kwenye hatua iliyofuata kwa sababu ya kiwango cha wachezaji wote.
“Leo (Messi) bila Neymar, bila Suarez, bila Iniesta, bila Pique, bila wachezaji wengine wote hawezi kuwa bora, pamoja na kwamba ni mchezaji bora sana.”
Taarifa ya klabu hiyo iliyotolewa Ijumaa iliyopita ilisema kuwa klabu hiyo imemuondoa Gratacos kutoka kwenye jopo la wakurugezi wa klabu hiyo. “Tumemfukuza kwa kutoa mawazo hadharani ambayo hayaendani na falsafa ya klabu hii,” ilisomeka taarifa hiyo.
Gratacos ni kati ya makocha ambao walifanikiwa kumfundisha Messi wakati akiwa kijana kwenye kikosi cha Barcelona kabla hajateuliwa kuwa mkurugenzi.