
HAKUNA jambo lingine ambalo Arsenal wanatakiwa kufanya leo Ijumaa zaidi ya kuhakikisha kuwa wanaibuka na ushindi dhidi ya Liverpool kwenye mchezo wa Ligi Kuu England ‘Premier League’.
Arsenal watakuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Emirates na ushindi tu ndiyo unaweza kuwapa matumaini ya kumaliza mwaka 2017 wakiwa kwenye nafasi ya nne za juu kwenye ligi hiyo kali barani Ulaya kwa sasa.

Arsenal wapo nafasi ya tano wakiwa nyuma ya Liverpool kwa tofauti ya pointi moja tu, baada ya Liverpool kukusanya pointi 34 na Arsenal kuwa na pointi 33 kwenye michezo 18.
Mchezo huu unaaminika kuwa utakuwa mkali na ushindani kwa timu zote baada ya Arsenal kuchapwa mabao 4-0 kwenye mchezo wa mzunguko wa kwanza uliopigwa kwenye Uwanja wa Anfield.
Kocha wa Liverpool, Juggen Klopp atakwenda kwenye mechi hiyo bila kuwa na wachezaji wake mahiri Alberto Moreno anayesumbuliwa na enka na Nathaniel Clyne (nyama), huku Daniel Sturridge na Joel Matip wakiwa na hatihati ya kuwepo.
Upande wa Arsenal wataingia uwanjani wakiamini kuwa hawawezi kumtumia mshambuliaji Olivier Giroud ambaye amekuwa akisumbuliwa na majeraha ya nyama za paja kuanzia alipoumia kwenye mchezo wa Carabao Cup katikati ya wiki dhidi ya West Ham.
Rekodi zinaonyesha Arsenal kwa sasa ni ‘nyanya’ kila anapokutana na Liverpool kwani kwenye michezo mitano ya mwisho ya Premier haijashinda mchezo hata mmoja.
Hata hivyo, hali halisi inaonyesha kuwa mchezo kati ya timu hizo mbili kuwa na mabao mengi jambo ambalo pia linaweza kutokea kwenye mchezo wa leo.
Liverpool wamekuwa na safu kali ya ushambuliaji, lakini ukitazama kwenye ulinzi bado mambo yao siyo mazuri kwa kuwa wame kuwa wakiruhusu mabao mengi.