×

CCM YASHINDA KWA KISHINDO SINGIDA, SONGEA NA LONGIDO

Dr. Damas Ndumbaro alipokuwa akitambulishwa kwa wananchi na Mwigulu Lameck Nchemba kabla ya kufanyika uchaguzi January 13, 2018.

KATIKA uchaguzi wa marudio uliofanyika jana nchini katika majimbo matatu ya ubunge, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeibuka kidedea  katika majimbo ya  Songea Mjini, Singida Kaskazini na Longido ambapo katika matokeo hayo Singida Kaskazini, kwa mujibu wa msimamizi, Rashid Mandoa, aliyeshinda nafasi hiyo ni Justine Monko aliyepata kura 20,857 ambazo ni  asilimia 93.5.

 

Wagombe wengine katika kinyang’anyiro hicho kutoka vyama vingine ni  Dalphine Mlewa wa CUF (974),  Aloyce Nduguta wa Ada-Tadea  (265), Omar Sombi wa AFP (116) na Mchungaji Yohana Labisu wa CCK kura 86.

 

Mandoa alisema kura zote kwa waliojiandikisha jimbo hilo ni   91,518,  ambapo watu 69,220 wanaofanyiza asilimia 70 hawakupiga kura.

 

Huko  Songea Mjini, msimamizi wa uchaguzi, Tina Sekambo alimtangaza Dkt.  Damas Ndumbaro kuwa mshindi kwa kuibuka na kura  45,762 ambazo ni asilimia  97.

 

Aliyeshika na fasi ya pili ni  Christina Thinangwa wa CUF aliyepata kura 608 ambapo Neema Tawete wa ADA-TADEA akipata kura  471.  Waliojiandikisha kupiga kura walikuwa ni 128,841.

 

Huko Longido  msimamizi wa uchaguzi, Jumaa Mhina, alimtangaza Dkt. Stephen Kiruswa, kushinda kwa kupata kura 41,258 ambazo ni asimilia 99.1.