
KLABU ya Majimaji ya Songea imeungana rasmi na Njombe Mji kuteremka Ligi Kuu Bara mpaka daraja la kwanza baada ya kulazimishwa sare ya bao 1-1 na Simba SC.
Katika mchezo huo uliopigwa Uwanja wa Majimaji mjini Songea, Ruvuma, Majimaji ilijiandika bao lake kupitia kwa Marcel Kaheza huku Niyonzima akisawazisha mnamo dakika ya 45 kwa njia ya penati.
Niyonzima alifunga penati hiyo baada ya beki wa Majimaji kuunawa mpira uliopigwa na Mohammed Ibrahim eneo la hatari.
Matokeo hayo yameishusha rasmi Majimaji iliyokuwa inaombea Ndanda ipoteze wakati ikipiga dua ipate ushindi kwa Simba lakini mambo yamekuwa kinyume.
Wakati huo Ndanda FC imesalia rasmi katika ligi baada ya ushindi mnono wa mabao 3-1 dhidi ya Stand United katika mchezo uliopigwa mjini Mtwara kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona.
Ndanda imesalia ikiwa na alama 29 na Majimaji ikishuka ikiwa ina pointi 25 na Njombe Mji FC iliyokuwa ya kwanza kuaga Ligi Kuu ikiwa na alama zake 22.