
STAA wa Bongo Fleva, Naibu Abdul ‘ Diamond Platinumz’ amefanya sapraizi ya aina yake na kuwashangaza mashabiki zake baada ya kuibuka kwenye shoo ya Usiku wa Kusini ‘Kusi Night’ iliyofanyika usiku wa kuamkia leo katika Ukumbi wa Dar Live, Mbagala Zakeem, jijini Dar es Salaam.

Shoo hiyo iliyokuwa maalum kwa Harmonize, ilimfanya Diamond ashindwe kujizuia na kutoka huko alikokuwa usiku wa manane kisha kuvamia steji ya Dar Live na kugonga nyimbo mbili ukiwemo mpya alioshirikishwa na Harmonize unaoitwa Kwangwaru. Katika taharuki ya furaha iliyotokea, mashabiki walishindwa kuelewa ‘King Mond’ alikuwa kaibukia wapi.

Baada ya Diamond kuvamia jukwaa, mashabiki walilipuka kwa shangwe ambapo staa huyo aliungana na Harmonize huku shoo ikianza upya. Mashabiki walipagwa na burudani ikanoga kwani hakuna aliyefahamu endapo Mond angefanya sapraizi kama hiyo. Mmanyema (Diamond) na Mmakonde (Harmonize) wakaliamsha dude ambapo kila mtu aliona kwamba haikuwa kazi ya kitoto.

Ikumbukwe kwamba jukwaa la Dar Live ndilo lilianza kuonyesha njia ya mafanikio ya muziki wa Harmonize mwaka 2015 baada ya kupewa nafasi na Diamond ya kuimba kwenye jukwaa hilo, ndipo kipaji chake kilionekana na Mond akamchukua.Usiku wa kuamkia leo ulikuwa ni kumbukumbu muhimu kwa wawili hao kukutana tena jukwaa moja lililowakutanisha siku ya kwanza. Mbali na hivyo, ilikuwa siku muhimu ya Harmonize alivyoanza safari yake ya muziki.

