
Mbunge wa Mchinga (CUF), Hamidu Bobali, ametolewa nje ya ukumbi wa Bunge leo Alhamisi Juni 28, 2018 na Spika Job Ndugai.
Ndugai amechukua uamuzi huo baada ya kuibuka mvutano kati yake na mbunge huyo.
Mvutano huo ulianza baada ya Bobali kusimama na kumpa taarifa Mbunge wa Siha (CCM), Dk. Godwin Mollel, aliyekuwa akichangia Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2018, kuunga mkono kufutwa kwa kifungu cha 17A cha Sheria ya Sekta ya Korosho ili kuruhusu ushuru unaotokana na mauzo ya korosho ghafi nje ya nchi kuingizwa katika Mfuko Mkuu wa Serikali.
Wakati Bibali akiendelea kutoa taarifa yake kwa Dk. Mollel, Ndugai alimtaka akae chini kwa maelezo kuwa anachokizungumza hakina uhusiano na anachokieleza mbunge huyo wa Siha.
Bobali kabla hajamaliza kumpa taarifa Dk. Mollel, spika alimtaka Bobali kukaa chini kwa kile alichomweleza kwamba anachokizungumza hakikuwa na uhusiano na alichochangia Dk. Mollel.
Mara baada ya Bobali kuketi, Ndugai alimtaka aheshimu kikao cha Bunge.
Baada ya kumtaka Mollel kuendelea na mchango wake, Ndugai alisema, “mheshimiwa Bobali toka nje tukutane mkutano ujao wa Bunge.”