
MSHAMBULIAJI mpya wa Simba, Mnyarwanda, Meddie Kagere ametamba kasi hiyo ya kufumania nyavu aliyoianza kwenye michuano ya Kombe la Kagame, amepanga kuendelea nayo kwenye msimu ujao wa Ligi Kuu Bara.
Hizo ni salamu kwa mabeki wa timu pinzani wa Yanga, Kelvin Yondani, Vincent Andrew ‘Dante’ na Azam FC, Aggrey Morris katika kuelekea kwenye msimu ujao.
Mnyarwanda huyo alijiunga na Simba hivi karibuni akitokea Gor Mahia ya nchini Kenya baada ya mkataba wake kumalizika ambaye hadi hivi sasa amefanikiwa kufunga mabao matatu katika michezo minne aliyocheza ya Kombe la Kagame ambayo leo inafikia fainali kwa Simba kucheza na Azam FC.

Akizungumza na Championi Ijumaa, Kagere alisema amekuja kuichezea Simba kwa ajili ya kuipa mafanikio pekee na siyo kitu kingine kwa kuhakikisha anaifungia mabao timu yake hiyo mpya.
Kagere alisema anafurahia ushirikiano mzuri aliokuta Simba kwa kuanzia kwa wachezaji, viongozi na mashabiki ambao walimpokea vizuri, hivyo amepanga kutowaangusha na kuthibitisha ubora wake kwa kuendelea kufunga zaidi.
Kitu ninachokiomba hivi sasa kutopata majeraha pekee, kila siku ninamuomba Mungu nisipate majeraha kwani yataharibu malengo yangu niliyoyapanga nikiwa na Simba.
“Kikubwa ninataka kutimiza malengo yangu yote niliyojiwekea nikiwa na Simba na kati ya hayo kuipa makombe ikiwemo hili la Kagame ambalo tayari tumeingia fainali ya michuano hiyo.
“Baada ya Kagame nguvu zake nitazielekeza kwenye ligi kwa kuendelea kufunga zaidi mabao na katika hilo ninaamini nitafanikiwa kutokana na ushirikiano mkubwa ninaoupata Simba kutoka kwa wachezaji.
“Mashabiki wa Simba watarajie mengi mazuri kutoka kwangu, kwani ninawapenda sana nimekuja kuwapa furaha,” alisema Kagere.
Stori: Wilbert Molandi, Championi Ijumaa
