






MAHAKAMA Kuu, Kanda ya Tanga imewapongeza baadhi ya Watumishi wake waliofanya vizuri kwa kuwapa vyeti maalum ikiwa ni ishara ya kutambua mchango pamoja na juhudi zao katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
Vyeti hivyo vilitolewa kwa watumishi hao na mgeni rasmi ambaye alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Bw. Martine Shigela, Agosti 24, 2018 katika hafla fupi ya kuwaaga Majaji na Mahakimu waliohamishwa vituo pamoja na watumishi wa kada mbalimbali waliostaafu.
Utaratibu huu umeanzishwa katika kanda hii ili kuenzi jitidaha na ufanisi wa kazi waliokuwa nao kipindi cha utumishi wao.
Miongoni mwa Watumishi waliopatiwa vyeti hivyo ni pamoja na Mahakimu wa Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo, Maafisa Utumishi, Wasaidizi wa Kumbumbuku, Wahasibu, Makatibu Mahsusi, Madereva, Walinzi, Mahakama za Wilaya zilizofanya ukarabati mkubwa wa Mahakama za Mwanzo, Kituo kilichoongoza kwa watumishi wake kuvaa sare na kuonekana nadhifu pamoja na Mahakama za Wilaya na Mwanzo zilizosikiliza na kuamua mashauri kwa asilimia nyingi kuliko zingine.
Watumishi waliostaafu ambao waliagwa katika hafla hiyo ni Bwana. Jumbe Athumani Kai, Msaidizi wa hesabu, Mahakama ya Wilaya Korogwe, Bi. Lydia Yohana Andrew Msaidizi wa kumbukumbu, Mahakama ya mwanzo Mashewa Wilayani Korogwe na Bi. Shehu Ally Muhsin, Msaidizi wa kumbukumbu Mahakama ya Wilaya ya Tanga.
Viongozi wengine waliohudhuria katika hafla hiyo ni pamoja na Mkuu wa chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto IJA, Mhe Jaji Faustine Kihwelo, Mkuu wa Wilaya wa Handeni, Mhe. Godwin Gondwe, Mkuu wa Wilaya ya Kilindi, Mhe. Sauda Mtondoo, Mkuu wa Wilaya ya Korogwe, Mhe. Kissa Gwakisa Kasongwa, Mkuu wa Wilaya ya Tanga, Mhe. Thobias Mwilapwa, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji – Korogwe, Nicodemus John, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga Benedict Wakulyamba.
Na Amina Ahmad, Mahakama Kuu-Tanga