MAMBO yakiwa moto Ligi Kuu Bara kiungo mahiri wa klabu ya Simba, Mzambia Claytous Chama ameonekana bora kitakwimu na kuweza kumfunika kiungo tegemeo wa Yanga, Feisal Salum ‘Fei Toto’ baada ya kucheza michezo kadhaa ya ligi ikiwa tu ndiyo mara yao ya kwanza kucheza ligi hii.
Chama ambaye amekuwa akiibeba Simba amefanikiwa kuichezea timu hiyo jumla ya mechi nane kati ya kumi ambazo timu hiyo imecheza mpaka sasa kwenye ligi.
Michezo hiyo ni Simba dhidi ya Yanga (0-0), Ndanda (0-0), African Lyon (2-1), Stand United (3-0), Mwadui FC (3-1), Alliance (5-1), Ruvu (5-0) na mechi dhidi ya Mbao ambayo Simba ilipoteza kwa bao 1-0.
Mbali na mechi hizo nane ambazo amecheza amekosa michezo miwili ile ya kwanza dhidi Tanzania Prisons pamoja na Mbeya City kutokana na ITC yake kuchelewa kufika.
Chama amefanikiwa kufunga ambao mawili msimu huu moja kwenye mchezo dhidi ya Stand na lingine dhidi ya Alliance Schools.
Katika michezo ambayo amecheza Chama mchezo dhidi ya Ndanda FC ndiyo aliweza kuanzia benchi na katika michezo yote nane amefanikiwa kutoa asisti mbili ambazo alitoa mchezo dhidi ya Stand akitoa pasi ya mwisho kwa Emmanuel Okwi na mchezo dhidi ya Alliance alitoa asisti kwa Adam Salamba.
Lakini kwa upande wa kiungo Feisal Salum Fei Toto msimu huu tangu amejiunga na Yanga amefanikiwa kucheza mechi saba na kukosa mchezo mmoja pekee dhidi ya Alliance baada ya kuwa na adhabu ya kadi.
Fei Toto amecheza mechi dhidi ya Simba (0- 0), Mtibwa Sugar (2-1), Stand United (4-3), KMC (1-0), Mbao (2-0), Coastal Union (1-0) na Singida United (2-0) na hawajapoteza mchezo wowote.
Lakini amefanikiwa kufunga bao moja katika mechi yao na KMC ya ushindi wa (1-0) na hajatoa asisti yoyote katika michezo ambayo amecheza na hakuna mchezo ambao aliweza kutokea benchi yote ameanza moja kwa moja.
Chama na Fei Toto wamejiunga na klabu hizo msimu huu wakitokea klabu tofauti na wamekuwa gumzo kutokana na viwango ambao wamekuwa wakionyesha katika michezo tofauti.
Martha Mboma, Dar es Salaam