
MKUU wa Wilaya ya Kisarawe, Jokate Mwegelo, amesema mgeni rasmi katika kampeni kabambe ya Tokomeza Ziro itakayofanyika Machi 30 mwaka huu katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam atakuwa Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassani.
Akizungumza na Global TV leo, Jokate aliwaomba Watanzania kujitokeza kwa wingi siku hiyo ya Machi 30 mwaka huu kwenye kampeni hiyo kabambe inayolenga kuleta maendeleo ya elimu wilayani Kisarawe.

Alisema kampeni hiyo inakusudia kuchangisha fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule ya sekondari ya wasichana wilayani Kisarawe, mkoani pwani.
Alisema siku hiyo kutakuwa na mambo mengi ndani ya ukumbi huo na amewaomba Watanzania kujitokeza kwa wingi kwa sababu elimu ikitolewa kwa mtoto wa Kisarawe ni faida kwa taifa zima.

“Tokomeza ziro ni kampeni ya kuhakikisha tunapanua elimu wilayani Kisarawe na tunaanzia kwa kujenga shule hiyo ya wasichana, niwaombe wote wenye kutaka maendeleo ya elimu wajitokeze siku hiyo pale Mlimani City,” alisema mkuu huyo wa wilaya.
Alibainisha kuwa moja ya vipaumbele alivyojiwekea tangu ateuliwe na Rais John Magufuli kuongoza wilaya hiyo ni kusukuma mbele maendeleo ya elimu kwa wasichana na wavulana.

“Kuna changamoto nyingi kama vile mimba za utotoni kwa wasichana lakini tukijenga mabweni, tutakuwa tumepunguza tatizo kwa kiasi kikubwa,” alisema Jokate na kusisitiza kuwa ni matarajio yake kuwa siku hiyo watu wengi watajitokeza ambapo meza moja itauzwa kwa shilingi milioni moja.

PICHA NA MUSA MATEJA | GPL