
ILE rufaa ya Yanga waliomkatia kocha wake, Mwinyi Zahera, kupinga faini aliyopigwa ya kutoa shilingi laki tano na kusimamishwa mechi tatu imekwama kutokana na kutopewa majibu hadi leo.
Hivi karibuni Bodi ya Ligi ilimfungia Zahera kusimamia mechi tatu kutokana na kutoa lugha chafu kwa bodi hiyo pamoja na kupigwa faini ya shilingi laki tano kwa kutovaa nadhifu.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Frederick Mwakalebela amefunguka kuwa rufaa waliyoiwasilisha kwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), wiki iliyopita juu ya kocha wao, bado haijajibiwa hadi sasa.
Aidha, Yanga walikata rufaa kutaka Bodi ya Ligi na TFF kumuita kocha huyo aweze kujieleza kabla ya kutoa hukumu kwa kufuata kanuni za TFF na sheria za nchi.
“Bado tunaendelea kusubiria rufaa yetu tuliyoipeleka TFF ambayo bado haijajibiwa, hivyo tukipewa majibu ndiyo tutajua nini cha kufanya,” alisema Mwakalebela.