×

Kocha wa Yanga Apewa Mbinu Tatu na Chama

Mwinyi Zahera

KIUNGO mchezeshaji wa Simba, Mzambia Clatous Chama amewaambia Yanga pamoja na kocha wao Mwinyi Zahera kuwa kama wanataka kushinda katika Uwanja wa Levy Mwanawasa uliopo Zambia basi wanatakiwa kutulia na kuacha kucheza kwa presha.

 

Chama amewapa mbinu hizo Yanga ikiwa wanajiandaa kucheza na wenyeji wao Zesco United kwenye pambano la Ligi ya Mabingwa Afrika ambalo litapigwa wikiendi hii katika uwanja huo ambao umekuwa machinjio kwa wageni wengi. Kiungo huyo ambaye ameichezea Zesco kabla ya kuja Bongo, amesema kuwa kitu pekee ambacho Yanga wanatakiwa kukifanya ni kucheza kwa kujiamini na kutulia muda wote wa mchezo.

 

“Ndiyo kweli pale Levy Mwanawasa mara zote Zesco wanapata ushindi kwenye mechi zao lakini niwaambie Yanga wakitaka kushinda basi kuna vitu vichache wanatakiwa kuvifanya.

 

“Kitu kikubwa kwanza wanatakiwa kujiamini, lakini pia wacheze kwa kutulia na kutofanya makosa kwani kama ikitokea wamefanya makosa wanaweza kujikuta wanawapa faida Zesco ya kushinda kwenye mechi hiyo, lakini pia wanatakiwa kupunguza presha kwa kuwa wenzao wapo kwao,” alisema Chama ambaye alifunga bao lililowaingiza Simba robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu uliopita.

Yanga wamefika kwenye hatua hii baada ya kuwachapa Township Rollers jumla ya mabao 2-1. Katika mchezo wa kwanza hapa nyumbani Yanga walifanya uzembe na kuruhusu bao mwishoni ambapo mchezo huo ulimalizika kwa sare ya bao 1-1. Mshindi wa mchezo huo kati ya Yanga na Zesco atatinga katika hatua ya makundi ya ligi hiyo kubwa zaidi kwa upande wa klabu na atakayepoteza ataangukia Kombe la Shirikisho kwa kucheza mechi za mtoano.