
Watoto wanaozaliwa na changamoto mbalimbali katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, wana kila sababu ya kupata ahueni mara baada ya wafanyakazi wanawake wa Benki ya Absa Tanzania, kukabidhi msaada wa vifaa tiba na vifaa muhimu vya kusaidia watoto hao wanaozaliwa kabla ya kufika wakati wa kujifungua.
Akizungumza wakati akipokea vifaa hivyo, Mkuu wa Kitengo cha Watoto Wachanga katika hospitali hiyo, Dk. Martha Mkony alitoa shukrani kwa wafanyakazi hao waliofika hospitalini hapo kama sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani akisema msaada huo umefika kwa wakati muafaka kwani utasaidia sana huduma za watoto hao wanaozaliwa kila siku katika hospitali hiyo.

“Nipende kuwashukuru sana wafanyakazi wanawake wa Benki ya Absa kwenye kundi lenu mnaloliita ‘Red Skirts’ kwa tendo hili la kijamii, na tunajua hii ni mwanzo wa mahusiano marefu kati ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kitengo cha watoto wachanga pamoja na Benki ya Absa na tunaahidi kushikiriana kwa pamoja katika kuwahudumia watoto wachanga”, alisema Dr. Marha.
Akizumgumza wakati akibidhi vifaa hivyo, Mkuu wa Kitengo cha Rasilimali Watu wa Benki ya Absa Tanzania, Bi. Martha Chacha alisema, kwa kuthamini mchango wa wanawake katika maendeleo ya Taifa, pamoja na changamoto mbalimbali zinazowakabili, wanawake wa Benki ya Absa Tanzania, kupitia umoja wao wa ‘Red Skirts’ walikwenda kutoa misaada kwa wagonjwa wa fistula katika Hospitali ya CCBRT pamoja na kitengo cha Watoto Njiti katika Hospitali ya Muhimbili.
“Kwa niaba ya wanawake wenzangu wakati wa tunaadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, tupo mahali hapa tukiwakilisha benki yetu kutoa misaada hii, Benki ya Absa inajali Story za Wanawake wa Tanzania, Story za mafanikio ya kiafya na kiuchumi kwa wanawake zina umuhimu sana kwetu”, aliongeza Bi. Anna.
Ikizinduliwa jijini Dar es Salaam mnamo Machi 2020, Programu ya Red Skirts ilibuniwa ili kuhamasisha, kuwawezesha, na kuendeleza viongozi wanawake katika Benki ya Absa.