The House of Favourite Newspapers

BUKU TANO KUITAZAMA SIMBA IKIKIPA NA SEVILA TAIFA DAR -VIDEO

Shirikisho la soka nchini, TFF, limetangaza bei za viingilio kwa mchezo wa kimataifa utakaowakutanisha mabingwa wa Tanzania Bara, Simba SC na Sevilla FC kutoka nchini Hispania.

 

Mechi hiyo ya kukata na shoka inatarajiwa kupigwa siku ya Mei 23 kwenye dimba la Taifa jijini Dar es Salaam kuanzia majira ya saa 1:00 Usiku.

 

Akizungumza kwa niaba ya TFF, Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa shirikisho hilo, Ndugu Cornel Barnaba ametangaza bei za tiketi kuelekea mchezo huo.

 

“Kutakuwa na viingilio vya aina tatu, cha kwanza ni Sh 5000 kwa mzunguko na kingine ni 15000 kwa jukwaa la VIP B.

“Pia kutakuwa na kiingilio cha Platinum kwa gharama ya Tsh 100,000 ambapo walengwa watapewa usafiri wa kwenda uwanjani kutoka hoteli ya Serena na kurudishwa, tiketi za mechi pamoja na chakula na vinywaji wawapo uwanjani,” alisema.

 

Aidha Mkurugenzi huyo ametaja sehemu ambazo tiketi hizo zitauzwa huku akitoa rai kwa mashabiki kununua tiketi zao mapema ili kuepuka usumbufu.

 

“Tiketi zitauzwa kwenye vituo vya mafuta vya Puma kote jijini Dar es Salaam ambapo utaweza kununua kupitia kadi yako ya Selcom hivyo watu waanze kununua tiketi mapema ili kuepuka uwezekano wa kukosa tiketi mwishoni,” alihitimisha Barnaba.

 

Mkurugenzi wa Utawala na Udhibiti wa kampuni ya SportPesa, Ndugu Tarimba Abbas akizungumza na wanahabari kwenye makao makuu ya TFF leo wakati wa utangazwaji wa bei za viingilio vya mchezo kati ya Simba na Sevilla (Picha na SPN)

 

Futari Uwanjani

Akizungumza kwenye mkutano huo na waandishi wa habari uliofanyika katika makao makuu ya TFF jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Utawala wa Udhibiti wa SportPesa, Ndugu Tarimba Abbas amesema wamemua kuweka mechi jioni ili kutoa fursa kwa kila mtanzania kuja kushuhudia.

 

“Tunajua mechi itachezwa wakati wa Mfungo wa Ramadhan hivyo tumeamua kuruhusu wajasiriamali wanaouza futari kuja kuuzia uwanjani ili watu wapate kufuturu kabla ya kuingia kwenye mechi.

 

Sevilla wanatarajiwa kutua nchini kwa ajili ya ziara ya mwisho wa msimu ambapo sambamba na kuwavaa Simba Mei 23, lakini pia mabingwa hao mara tano wa UEFA Europa League watatembelea vivutio mbalimbali vya utalii nchini, kushiriki katika kliniki za soka na semina za mafunzo kwa viongozi wa soka nchini.

Comments are closed.