The House of Favourite Newspapers

Messi Ainyamazisha Santiago Bernabeu Kibabe, Waipiga Madrid Bao 3-2

0
Nyota wa Dunia, Lionel Messi akishangilia baada ya kupiga bao la tatu.

Barcelona imepata ushindi wa mabao 3-2 katika mchezo unaojulikana kwa jina la El Clasico ambapo walikuwa wababe dhidi ya Real Madrid katika Ligi Kuu ya Hispania ‘La Liga’.

Lionel Messi ndiye aliyekuwa shukaa katika mchezo huo kutokana na kuonyesha kiwango cha hali ya juu akimfunika mpinzani wake Cristiano Ronaldo wa Madrid.

Barcelona imepata ushindi huo usiku wa jana kwenye Uwanja wa Santiago Bernabeu na kusababisha mashabiki wengi wa Madrid kuwa kimya kwa kuwa wao ndiyo waliokuwa wengi na walikuwa wakishangilia zaidi ya wenzao waliokuwa wachache.

Mtifuano ukiendelea.

Lionel Messi ndiye aliyekuwa hatari zaidi kwa Madrid baada ya kufunga mabao mawili katika dakika ya 33 na dakika ya 90 huku Ivan Rakitic akifunga katika dakika ya 73.

Wachezaji wa Barcelona wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ushindi.

Ushindi huo wa Barcelona ulikuja kwa timu hiyo kulazimika kutoka nyuma na kushinda baada ya wenyeji kutangulia kupata bao kupita kwa Casemiro katika dakika ya 28 huku bao lao la pili likifungwa na James Rodriguez dakika ya 86.

Kwa ushindi huo Barcelona imeifikia Madrid kwa timu zote kuwa na pointi 75 licha ya kuwa Madrid ipo nyuma kwa mchezo mmoja, ikiwa na maana kuwa mbio za ubingwa zimerejea kwa timu zote.

Katika mchezo huo, Madrid ilimuanzisha Gareth Bale aliyekosa mechi mbili zilizoputa kutokana na kuwa majeruhi lakini alishindwa kuendelea baada ya kuonekana ana maumivu dakika ya 39 na nafasi yake kuchukuliwa na Marco Asensio.

Katika dakika ya 20, Lionel Messi alilazimika kucheza akiwa na pamba maalum mdomoni baada ya kupigwa kiwiko mdomoni na beki wa Real Madrid, Marcelo wakati wakiwania mpira.

Messi alilazimika kupata matibabu kwa dakika kadhaa nje kwa kuwa alikuwa akitokwa na damu mdomoni lakini aliporejea aliendelea kuonyesha makali yake ya kukokota.

Leave A Reply