Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolijia Mhandisi Stella Manyanya leo amekabidhi Bendera ya Taifa kwa wanafunzi Watanzania kwenda kuipeperusha Tanzania katika Mashindano ya Ubunifu yajulikanayo kama ‘First Global Robotic Challenge’ yanayotarajiwa kufanyika nchini Marekani hivi karibuni.
Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika kwenye shule ya wasichana Jangwani jijini Dar, Manyanya alisema mashindano hayo yanatarajiwa kuzikutanisha zaidi ya nchi 150 na kwa Tanzania washiriki wametoka kwenye shule mbalimbali na watakutana kubuni kutengeneza Roboti.
“Kutokana na ushiriki wa wanafunzi hawa waliotengeneza roboti hii kupitia mfumo wa kisayansi yenye mfumo wa utambuzi hakika ni ishara tosha kwa vijana wetu, tuwatie moyo ili wakafanye vizuri huko waendako na kutuletea ushindi,”alisema Manyanya.
Aidha amewahimiza wanafunzi wa Shule ya Sekondari Jangwani, Dar kuzingatia masomo ili waweze kutimiza ndoto zao, badala ya kujiingiza katika mapenzi wakati wangali shuleni.
Aliongeza kuwa Rais Magufuli anapaswa kuungwa mkono kwa kutoruhusu wanafunzi wanapopata mimba na kujifungua kurudi shuleni.