
SWALI la Mbunge wa Konde (CUF), Khatib Said Haji kuhusu upungufu wa nguvu za kiume kwa wanaume nchini, limewaibua wabunge wengine wakitaka kuuliza maswali ya nyongeza, ingawa Naibu Spika, Dk Tulia Ackson hakuwapa nafasi.
Mbunge huyo ametaka kujua kuhusu ongezeko la wanaume wanaopungukiwa nguvu za kiume, hivyo kuhoji iwapo Serikali inalijua tatizo hilo.
“Kama jibu ni ndiyo, je, Serikali inachukua hatua gani kukabiliana na tatizo hilo ambalo linaondoa amani ndani ya nyumba na kwa nini Tanzania imekuwa ya kumi duniani miongoni mwa nchi zilizopoteza furaha?” alihoji Haji.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Afya, Dk Hamisi Kigwangalla amesema Serikali inalitambua tatizo hilo japokuwa hakuna jibu la moja kwa moja kwa kuwa tendo la ndoa ni siri kati ya wanandoa wenyewe.
Dk Kigwangalla ametaja baadhi ya sababu za kupungua nguvu za kiume ni umri wa zaidi ya miaka 60, maradhi sugu, kifua kikuu, kisukari, kansa, ukimwi na wanaotumia dawa muda mrefu.
Kuhusu wauza dawa zinazoelezwa kuwa zinaongeza nguvu za kiume, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu ameagiza waganga wakuu wa mikoa kuwakamata wote ambao wanafanya hivyo na hawana vibali kutoka mamlaka husika.
TAZAMA VIDEO WABUNGE WAKIHOJI