Kutana na George Majaba, Mshindi wa Nyumba ya Global Publishers
Hatimaye George Majaba, mkazi wa Dodoma, Mshindi Bahati Nasibu ya Shinda Nyumba iliyokuwa ikiendeshwa kwa zaidi ya miezi 6 na Kampuni ya Global Publishers, amepatikana na kuzungumzia furaha aliyonayo, baada ya kuibuka mshindi na kujinyakulia nyumba.
Majaba ambaye ni kondakta wa mabasi mjini Dodoma, aliibuka mshindi katika droo kubwa iliyofanyika kwenye Viwanja vya Las Vegas, Mabibo jijini Dar huku mgeni rasmi akiwa ni Diwani wa Kata ya Mabibo, Kassim Lema ambapo kuhusiana na ushindi wake, amesema furaha aliyonayo haielezeki.
Akizungumza na mwandishi wetu, Majaba amesema bado haamini macho yake kama kweli ameshinda kwa sababu alijaza kuponi kama kujaribu tu na wakati akijaza, mwanaye alimtabiria kwamba atakuwa mshindi lakini mwenyewe akamjibu ‘toa uchuro wako hapa’.
Majaba, baba wa familia ya watoto watatu, anasema maisha yake mpaka sasa, anaishi kwenye nyumba ya kupanga na familia yake na kwamba ushindi alioupata, umeyabadilisha kabisa maisha yake.