
NI SIMANZI, majonzi na vilio vimeikumba tasnia ya habari kufuatia kumpoteza mwanahabari mwenzao, Justine Limonga ambaye mwili wake umeagwa leo katika Viwanja vya Mbagala Zakhem jijini Dar es Salaam.


Katika tukio hilo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Hamphrey Polepole, ameongoza mamia ya waombolezaji wakiwemo wanahabari, ndugu, jamaa na marafiki katika ibada ya kuaga mwili wa mwanahabari huyo.

Akizungumza katika ibada hiyo, Polepole alisema CCM na tasnia ya habari imepoteza mtu muhimu ambaye alikuwa bado akitegemewa. “Tumempoteza mtu muhimu ambaye alikuwa akitegemewa kama chama tutaangalia namna ya kuisaidia familia yake,” alisema Polepole.

Akizungumzia msiba huo, Mkurugenzi wa Nduvini Auto Garage, Alhaji Ahmed Msangi alifafanua Limonga enzi za uhai wake na kuahidi katika kipindi hiki cha kufunguliwa kwa shule, kmpuni yake itawanunulia vifaa vya shule, sare na kuwalipia karo wakati wakisubiri kukaa na familia kuona namna ya kuwazesha kielimu watoto wa marehemu.

Kaimu Mkurugenzi wa Uhuru FM, Angel Akilimali alisema kifo cha mwanahabari huyo aliyekuwa mwajiriwa wao kimeacha pengo kubwa ambalo halitazibika.

Alisema Limonga alikuwa mhariri na mbunifu na aliweza kuongoza vipindi mbalimbali ambavyo vilipendwa na wasikilizaji wa Uhuru FM ambapo aliahidi stahiki zote za marehemu kama mwajiriwa zitapatikana kwa wakati.

Katika ibada hiyo iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, dini, siasa wanamuziki na wanahabari na wananchi iligubikwa na majonzi na baadhi ya watu kushindwa kujizuia kulia.

Akitoa mahubiri kwenye ibada hiyo Katekista wa Parokia ya Kutukuka kwa Msalaba Kizuiani, Philo Mbunda alisema mwenzetu Limonga amemaliza kazi ya hapa duniani je sisi tuliobakia tumejiandaeje?

Mbunda alisema kila mtu anapaswa kujitafakari maisha yake ya kiroho kabla ya kifo na hivyo ndivyo Mungu wetu anavyohitaji.

Limonga alifariki dunia Desemba 30, mwaka jana katika Hospitali ya TMJ alikolazwa akitibiwa na ameacha mjane na watoto wawili ambapo mazishi yake yamefanyika leo katika Makaburi ya Saku yaliyopo Chamazi nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.





