
KAMPUNI ya Msama Promotion inayoandaa Tamasha la Pasaka nchini ambalo ni la nyimbo za muziki wa Injili linalotarajiwa kufanyika Aprili Mosi na Pili katika Kanda ya Ziwa litahamia mkoa wa Dodoma ikiwa ni mkoa mwingine ambao umeongezeka kwa ajili ya tamasha hilo.
Mkoani Dodoma, Tamasha la Pasaka litafanyika Aprili 8 mwaka huu kwenye Uwanja wa Jamhuri ambapo mgeni rasmi wa tamasha hilo atatajwa baadaye.
Akizungumzia maandalizi ya tamasha hilo mkurugenzi wa kampuni hiyo , Alex Msama, amesema yamekamilika kwa kiwango kikubwa na kilichobaki ni wasanii kuwasili Mwanza kwa ajili ya kutoa burudani kwenye Uwanja wa CCM Kirumba Aprili Mosi na baadaye Aprili 2 kwenye uwanja wa Halmashauri mjini Bariadi mkoani Simiyu.
Msama amesema waimbaji wote wamethibitisha kushiriki matamasha ya Mwanza na Simiyu na wana kiu kubwa ya kutoa burudani kwa wakazi wa Kanda ya Ziwa na Kati mkoani Dodoma.
NA DENIS MTIMA/GPL