


MBUNGE na Naibu Waziri wa Mifugo na uvuvi, Abdallah Ulega, jana alipokea mifuko 200 ya saruji yenye thamani ya shilingi milioni tatu kutoka Shirika la Bima la Taifa kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati.
Akizungumza wakati akipokea saruji hizo alisema, zitatumika katika ujenzi wa zahanati katika vijiji mbalimbali kama Kibamba, Kazole, Yavayava na Mkanonge wilayani humo.
Ulega ameeleza kuwa kazi hii ni yetu sote katika kuunga mkono jitihada za Rais Magufuli na kuifikisha Tanzania mbele zaidi.
Pia ulega ameeleza kuwa ujenzi wa miundombinu hasa ya madarasa na zahanati unaendelea katika vijiji mbalimbali na hii ni katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma zote za msingi.
Aidha ameshukuru shirika hilo kwa msaada huo wa kusaidia Wilaya ya Mkuranga kwa ujenzi wa shule na zahanati.
Kwa upande wake Meneja Masoko wa Shirika la Bima la Taifa, Elisante Maleko ameeleza kuwa utoaji wa mifuko hiyo ya saruji ni kutokana na mahusiano mazuri baina yao hivyo wakaona faida wanayopata kutoka kwa wananchi hao ambao ni wateja wazuri ni kushiriki katika ujenzi wa miundombinu ya madarasa na zahanati katika vijiji mbalimbali vya Mkuranga.
Mkurugenzi wa shirika hilo tawi la Ubungo Segeja Mabulla amemshukuru mbunge na mkuu wa wilaya hiyo kwa kuwakutanisha na kutoa elimu ya kuwasaidia wananchi kuhusiana na masuala ya bima pia amewapongeza wakazi wa wilaya hiyo kwa kuwa wateja wazuri wa bima za halmashauri na bima za maisha.