WATANGAZAJI wa Clouds Media, Soudy Brown, Shaffih Dauda, msanii Maua Sama, mpigapicha, MX, mshereheshaji (MC) Luvanda na watuhumiwa wengine, leo wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam kusomewa mashitaka yanayowakabili.
Ijumaa iliyopita mmoja kati ya mawakili wa wahutumiwa hao, Jebra Kambone, alifungua kesi mahakamani hapo kuwaombea wateja wake hao dhamana baada ya kushikiliwa na Jeshi la Polisi kwa wiki moja katika Kituo Kikuu cha Polisi jijini Dar es Salaam.

Imeelezwa kuwa Hakimu atakayesikiliza shauri hilo namba 13 la mwaka 2018 ni Hakimu Mkazi, Huruma Shaidi.
Soudy Brown na Maua Sama wanashikiliwa na jeshi hilo kwa tuhuma za udhalilisha wa nembo ya taifa baada ya kusambaa clips za video zinazowaonyesha watu wakichezea pesa halali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Watuhumiwa wengine wanashikiliwa na jeshi hilo kwa kosa la kuchapisha maudhui kwenye mitandao ya kijamii wanayomiliki (Blogs na YouTube) bila kuwa na kibali kutoka Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA).
