
MWENYEKITI wa Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Wakili Revocatus Kuuli leo amejiuzulu kuongoza kamati na uongozi wa shirikisho hilo umesema kujiuzulu kwake siyo tatizo kwao kwani kazi zitaendelea kama kawaida.
Kuuli amejiuzulu nafasi hiyo ikiwa ni siku chake tangu Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidau, amwandikie barua ya kujieleza ndani ya siku tatu kwa nini amesimamisha uchaguzi wa klabu ya Simba.
Hata hivyo, katika taarifa ya Kuuli alisema tarehe ya uchaguzi ya Simba itabaki ileile iliyopangwa na Kamati ya Uchaguzi ya klabu hiyo ila wafanye marekebisho ya baadhi ya kanuni ambazo zipo kinyume na kanuni za uchaguzi za TFF.
Kuuli ameweka wazi kuwa hawezi kuendelea kuongoza kamati hiyo kwa kile alichodai ni kuwepo na ubabaishaji na kuingiliwa na majukumu ya kamati wakati yeye anasimamia sheria.
Makamu wa Rais wa TFF, Athuman Nyamlani, alizungumzia kujiuzulu kwa Kuuli akisema hakutapunguza wala kuongeza jambo lolote ndani ya TFF.