The House of Favourite Newspapers

Baba Kanumba Amsaka Lulu

IKIWA ni siku moja imepita tangu msanii wa filamu za Kibongo, Elizabeth Michael ‘Lulu’ amalize kifungo cha nje alichokuwa amehukumiwa kwa kesi ya kumuua bila kukusudia aliyekuwa msanii maarufu wa filamu, Steven Kanumba, baba mzazi wa marehemu Kanumba, Charles Kanumba anamsaka Lulu kwa udi na uvumba.

 

Akizungumza na Risasi Mchanganyiko kwa njia ya simu, Jumatatu iliyopita, baba Kanumba alieleza kwamba anamsaka Lulu ili aweze kumpa nasaha zake kama baba pamoja na ujumbe aliopewa na babu wa Kanumba.

Baba huyo aliendelea kueleza kuwa siku chache kabla Lulu hajamaliza kifungo, alitokewa na babu wa Kanumba yaani baba yake mzazi ambaye alifariki wakati mwanaye Kanumba anazaliwa na kupewa jina lake.

 

Alisema, alimpa maelekezo anayotakiwa kuyafanya Lulu ili aweze kuendelea na maisha yake vizuri.

“Babu wa Kanumba alinitokea na kuniambia nimkumbushe Lulu atekeleze mambo ya kimila ambayo nimewahi kumwambia tena ya kwenda kaburini kwa Kanumba na kufanya usafi na kumuombea na hapo atakuwa ameondokana na kile kivuli cha marehemu.

 

“Wakati Lulu anafanya hayo anatakiwa awepo ndugu wa upande wa ukoo wa Kanumba ili kushuhudia na akimaliza hayo atakuwa yupo salama na hatapata mikosi tena kwenye maisha yake na kile kivuli cha Kanumba kitakuwa kimemuondoka lakini vinginevyo atapata taabu,” alisema baba Kanumba.

Hata hivyo, baba huyo alisema hamlazimishi Lulu kufanya hivyo kwa kuwa hayo siyo maneno yake ni mila na maelekezo ya babu Kanumba ndiyo yanamtaka hivyo.

 

“Sina kinyongo na Lulu, nimefurahi sana yeye kumaliza kifungo na ninamuombea mafanikio makubwa sana kwenye maisha yake, ninahitaji na ninamsaka sana kwa udi na uvumba maana nina mengi ya kumwambia kama mwanangu,” alisema baba Kanumba.

 

Novemba, 2017 Lulu alihukumiwa kifungo cha miaka miwili jela baada ya kukutwa na hatia ya kumuua Kanumba bila kukusudia lakini Mei, mwaka huu alibadilishiwa kifungo ambapo alipewa kifungo cha nje ambacho alikuwa akifanya usafi katika ofisi za Wizara ya Mambo ya Ndani zilizopo jijini Dar hadi alipomaliza juzi, Novemba 12.

Stori:GLADNESS MALLYA, RISASI MCHANGANYIKO

Comments are closed.