The House of Favourite Newspapers

RAIS MAGUFULI AAHIRISHA SHEREHE ZA UHURU 

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza kuhusu uamuzi wa Rais  Dkt. John Pombe Magufuli  wa kuahirisha Maadhimisho ya sherehe za Uhuru yaliyotarajiwa kufanyika  9 Desemba, 2018, Kwenye ukumbi wa Mkuu wMkoa wa  Lindi, Novemba 20, 2018. Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Lindi Godfrey Zambi.

 

Rais Dkt. John Pombe Magufuli ameahirisha maadhimisho ya siku ya Uhuru, Disemba 9, 2018 na fedha zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya kufanikisha shamrashamra hizo ameelekeza zitumike kujenga hospitali mkoani Dodoma ambayo itaitwa Uhuru Hospitali.

 

 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo (Jumanne, Novemba 20, 2018) na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Rais Dkt. Magufuli ameagiza kiasi cha shilingi milioni 995.182 zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya kufanikisha sherehe hizo zitumike kwa ajili ya ujenzi wa hospitali mkoani Dodoma.

 

Waziri Mkuu ametoa taarifa hiyo wakati alipokutana na viongozi waandamizi wa mkoa wa Lindi pamoja na wilaya zake katika kikao cha maandalizi ya shughuli za kuzima Mwenge kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi.

 

Amesema hospitali hiyo itakayojengwa katika eneo la kati ya barabara ya kwenda Hombolo na Chamwino  kwenye barabara ya kwenda Dar es Salaam itakuwa inawahudumia wakazi wa mkoa wa Dodoma pamoja na wananchi wengine watakaokuwa  mkoani humo.

 

Kadhalika, Waziri Mkuu amesema Rais Dkt. Magufuli amewaagiza wakuu wa mikoa na wilaya waandae matukio watakayoyatekeleza katika maeneo yao yatakayoashiria maadhimisho ya siku ya Uhuru. “Wanaweza kutumia siku hiyo kwa kufanya usafi maeneo ya wazi au kwenye hospitali.”

 

Kufuatia maagizo hayo, Waziri Mkuu amewataka wananchi katika maeneo yote nchini wajiandae kufanya shughuli mbalimbali za kijamii zitakazopangwa na wakuu wao wa mikoa na wilaya kufanyika katika maeneo yao.

 

IMETOLEWA NA: OFISI YA WAZIRI MKUU,

JUMANNE, NOVEMBA 20, 2018.

BREAKING: JPM Apiga ‘STOP’ Sherehe Za Uhuru!

Comments are closed.