The House of Favourite Newspapers

MAGUFULI AONGOZA WAKATOLIKI KUAGA MWILI WA ASKOFU CHENGULA

Rais  John  Magufuli leo Novemba 26, 2018 ameungana na maaskofu, mapadri, watawa na waumini wa Kanisa Katoliki kutoa heshima za mwisho kwa aliyekuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Mbeya Mhashamu Askofu Evaristo Chengula aliyefariki dunia  Novemba 21, 2018 katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete jijini Dar es Salaam alikokuwa akipatiwa matibabu.
Misa takatifu ya kumuaga marehemu Chengula iliyoongozwa na Askofu Mkuu Mwandamizi Jude Thadaeus Ruwa’ichi, imefanyika katika Kanisa la Mtakatifu Imakulata lililopo makao makuu ya Baraza la Maaskofu, Kurasini jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na rais mstaafu wa awamu ya tatu,   Benjamin Mkapa na mkewe Anna Mkapa.
Akizungumza baada ya misa hiyo Magufuli ametoa salamu za pole kwa maaskofu wote wa Kanisa Katoliki, mapadri, watawa, waumini wa Kanisa Katoliki Jimbo la Mbeya na Wakatoliki wote nchini kwa kuondokewa na kiongozi aliyekuwa akifanya vyema kazi yake ya kutangaza Injili.
Amesema pamoja na majukumu yake ya kutoa huduma za kiroho marehemu alisimamia ukweli ikiwemo kupinga hadharani ndoa na mapenzi ya jinsia moja licha ya kuwepo mashinikizo mbalimbali.
Akitoa salamu kwa niaba ya Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) Makamu wa Rais wa TEC Mhashamu Askofu Flavian Kasalla amemshukuru Magufuli kwa ushirikiano alioutoa wakati wa kuuguza na baada ya kifo cha Askofu Chengula na pia amewashukuru madaktari na wauguzi, viongozi na wote waliokuwa wakimuombea kabla na baada ya kifo.
Mhashamu Askofu Evaristo Chengula amefariki dunia kwa ugonjwa wa moyo na baada ya misa ya kumuaga mwili wake umesafirishwa kwenda Mbeya.
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
26 Novemba, 2018

Comments are closed.