The House of Favourite Newspapers

Kakolanya Mguu Mmoja Simba

Beno Kakolanya.

HABARI mbaya kwa mashabiki wa Yanga ni kwamba, kuna uwezekano kipa namba moja wa timu hiyo, Beno Kakolanya akatua Simba kabla ya dirisha dogo la usajili halijafungwa. Yanga wamekuwa wakichukulia suala la mchezaji huyo kama masihara kwa madai kwamba Simba ina makipa wengi haiwezi kumtaka Beno.

 

Habari za uhakika zinasema kwamba Beno anataka kung’oka Yanga kwa kigezo cha kutotimiziwa masharti ya mkataba wake kutokana na malimbikizo ya mishahara na stahiki zingine zaidi ya miezi minne.

Lakini habari ambazo Spoti Xtra imejiridhisha nazo ni kwamba mchezaji huyo huenda dakika yoyote akatangaza habari mbaya kwa Yanga ingawa ana mkataba nao ambao amepanga kuupangua kisheria chini ya usimamizi wa meneja wake ambaye ni Simba damu. Simba imepanga kumtoa kwa mkopo kipa wake namba mbili, Deogratius
Munishi ‘Dida’ pamoja na Said Mohammed ‘Nduda’ na kubakiwa na Aishi Manula pekee ambaye atasaidiana na Beno.

 

Licha ya kwamba wanataka kuimarisha safu ya ulinzi lakini habari za ndani zinasema kwamba, usajili huo una lengo la kudhoofishana kuelekea mbio za ubingwa na Kombe la FA.

“Baada ya kumalizana na Mbukinabe, Zana Oumar Coulibaly kwa ajili ya kuziba pengo la Shomari Kapombe, sasa umeanza mpango wa Kakolanya na utakamilika kisayansi,”alidokeza mmoja wa vigogo wa Simba.

 

Alipoulizwa Kakolanya kuhusiana na hilo hakutaka kusema chochote zaidi ya kusema kuwa, “Kwa sasa sipo tayari kulizungumzia hilo kwani nipo na meneja wangu kuna mambo nayashughulikia.”

 

Kwa upande wake meneja wa Kakolanya ambaye pia ni kiongozi wa Simba, Seleman Haroub alipoulizwa kuhusiana na suala hilo alisema kuwa: “Kakolanya bado ana mkataba na Yanga ila kuna mambo ya kimkataba ambayo hajatimiziwa, wao ndiyo wanaweza kusababisha akaondoka klabuni hapo.”

 

AACHWA DAR Kakolanya na Kelvin Yondani hawamo katika safari ya timu hiyo iliyokwea Pipa jana kwenda Mbeya. Kikosi cha Yanga kimeondoka jijini Dar jana kuelekea Mbeya kwa ajili yamaandalizi ya mchezo wake dhidi ya Tanzania Prisons katika mchezo utakaochezwa kesho katika Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

 

Yondani na Kakolanya hawajaitumikia timu hiyo tangu watoke Taifa Stars iliyokwenda kucheza na Lesotho wiki mbili zilizopita ambapo hadi sasa wamekosa mechi dhidi ya Mwadui, Kagera Sugar na JKT Tanzania.

 

Akizungumza na Spoti Xtra linalotoka kila Alhamisi na Jumapili, Mratibu wa Yanga, Hafidhi Salehe amesema kuwa, kikosi cha Yanga kimeondoka jana na wachezaji 20 huku wachezaji kadhaa wakibakia akiwemo Yondani na Kakolanya ambao hawakucheza michezo iliyopita.

 

“Miongoni mwa wachezaji ambao wamebakia jijini Dar ambao hawatokuwepo katika mchezo dhidi ya Prisons ni Kakolanya , Yondani na baadhi ya wachezaji wengine ambao tumewaacha kwa sababu tofauti

SWEETBERT LUKONGE NA KHADIJA MNGWAHI

Comments are closed.