HABARI za wakati huu, ningependa kuanza na msemo kutoka wa Swami Vibekananda aliyenena; “Take up one idea. Make that one idea your life. Think of it, dream of it, live on that idea. Let the brain, muscles, nerves, every part of your body, be full of that idea and just leave every other idea alone. This is the way to success. That is way great spiritual giants are produced.”
Akimaanisha kama utaamua kuchukua wazo moja na kuliwaza, kulitafakari na kuwa ndilo kitu cha muhimu kwako, basi mwisho wa siku utafanikiwa. Kwa ufupi ni kuwa kila mtu mkubwa duniani alianza na wazo fulani lililomfanikisha.
Iko hivi; yeyote ambaye huwa ana mawazo ya tofauti na yaliyotangulia kuliko wengine huwa anakuwa wa tofauti na atajikuta anapiga hatua kuliko wengine katika eneo lake. Aidha, uwe umeajiriwa, umejiajiri, mfanyabiashara, mwanasiasa au mwanafunzi; uwezo wako wa kuja na mawazo ya tofauti ndiyo kiini na chanzo cha mafanikio yako hasa baada ya kuingia kwenye mwaka mwingine wa 2019.
1: TAFUTA UHITAJI
Kila mafanikio ni matokeo ya
uhitaji wa watu. Kila unacholipia pesa, kwako ni UHITAJI na kwa unayempa pesa ni kuwa AMETATUA TATIZO lako.
Kwa maneno mengine. Kadiri unavyoweza kutatua matatizo MAKUBWA na MENGI ndivyo unavyopata vyanzo vya pesa zaidi. Kwa ufupi umaskini ni matokeo ya kukimbia kutatua matatizo na utajiri ni matokeo ya kukimbilia kutatua matatizo.
Leo ningependa tuangalie njia kadhaa za namna ya kupata mawazo yanayoweza kuwa chanzo cha kubadilisha maisha yako unapoamua kuyafanyia kazi.
Na hapa ningependa kuwakumbusha maneno ya William Cameron aliyesema; “Money never starts an idea; it is the idea that starts the money.”
Fedha haileti mawazo ila mawazo ndiyo huleta pesa, ndiyo maana kuna watu walishawahi kupata pesa nyingi ila kwa kukosa mawazo wamerudi katika kufeli na umaskini.
Hebu chukua dakika moja, jiulize; Katika mazingira niliyopo, je, kuna uhitaji gani ninaoweza kuutatua? Chukua note book yako na andika kabla hatujaendelea.
Hivyo basi angalia mazingira yanayokuzunguka, je, kuna uhitaji gani? Kama maji yanatoka mara moja kwa wiki mtaani kwenu, ukifanikiwa kununua simtank kadhaa na kuuza maji siku ambazo hayatoki hapo unakuwa umetatua tatizo na umepata pesa. Kama umegundua watu karibu na maeneo ya kwenu wanatumia gesi na hakuna duka la karibu, tafuta namna ya kuwa wakala wa kuuza, kadhalika na mahitaji mengine eneo ulilopo.
Naamini umepata mawazo kadhaa. Tutaendelea kujifunza kisha utabaki na wazo moja.
2: BORESHA WAZO LA MWINGINE
Kuna wakati mwingine hutahitaji kuanza na wazo jipya kabisa, badala yake utahitaji kuchukua wazo la mwingine kuliboresha. Kwa mfano badala ya mtu kuuza matunda na kuyamenya mtu anaponunua mwingine akaboresha akaamua kuyamenya kabisa kisha anayapaki vizuri tayari kwa kuyauza.
Chunguza kile ambacho kinafanywa na wengine kisha jiulize, hivi nawezaje kuliboresha wazo hili?
3: HAMISHA WAZO LA WENGINE NA LIPE UHALISIA WA MAZINGIRA YAKO
Kuna mawazo mengi yaliyofanikiwa leo ni matokeo ya mawazo yaliyohamishwa kutoka mahali pengine na yakapewa uhalisia wa mahali husika. X-Factor ya Uingereza imezaa Bongo Star Search, DECA na SONY Records label ndiyo leo tunaona WCB.
Jaribu kuangalia, kuna wazo gani ambalo unaweza kulichukua na ukaliwekea mazingira ya kwako na ukalifanyia kazi. Unaweza kulitoa nje ya Tanzania na ukalileta Tanzania au ukalitoa Dar na ukalipeleka katika mkoa unaoishi.
4: RAHISISHA MCHAKATO WA KITU AMA BIDHAA FULANI
Sasa hivi kila mtu anajitahidi kutumia teknolojia kuuza bidhaa au kutoa huduma. Kwa nini? Kwa sababu ya kurahisisha mchakato kwa wateja.Tunaishi katika ulimwengu ambao watu hupenda kutumia muda mfupi kupata huduma au bidhaa, hivyo unachotakiwa kufanya ni kuhakikisha kuwa hata kama unatoa bidhaa au huduma ileile kama wengine, jaribu kurahisisha.
Ndiyo maana visimbuzi wanaweka huduma zao kwenye MPESA, Tigopesa, Airtel n.k, wanachojaribu kufanya ni kurahisisha.
Ni rahisi kwa mama ntilie anayepeleka chakula maofisini na akaongeza gharama ya usafiri juu ya 500 kwa kila sahani kuliko auze bei ya chini huku akisubiri watu wamfuate kilometa moja kule anakouza.
Inawezekana unataka kufanya kitu ambacho kila mtu anafanya, swali ni je, unaweza kutoa urahisi gani utakaovutia wanunuaji wa huduma au bidhaa yako?
5: TENGENEZA UHITAJI
Hii si njia rahisi sana ila inawezekana. Inamaanisha kuna vitu vingi watu wanahitaji ila hawawezi kuvitumia hadi viwepo.
Kabla soda hazijaja watu walikuwa wanakunywa maji, kabla TV hazipo watu walikuwa ni radio tu na hakuna mtu alikuwa anadai TV kwa kuwa haikuwepo. Lakini leo ni kama vile haiwezekani kuishi bila TV. Kuna mtu siku moja akauliza; “Hivi wazee wa zamani waliishije bila simu? Miahadi walifanyaje wakifika Kariakoo na kila mtu yuko kona yake?”
Hii ina maana kuna mahitaji mengi bado yako ila watu hawawezi kuyadai au kuulizia hadi yatakapokuwepo. Zamani scrub hazikuwepo ukienda saloon, lakini siku hizi ni kama vile ni lazima kila ukinyoa utajikuta unataka kufanya na scrub, tena ina bei kubwa kuliko hata kunyoa kwenyewe!
Hiyo inamaanisha kuna wazo unaweza ukaja nalo watu wakaanza kuhitaji hata kama hawajawahi kujua kama wanahitaji.
HITIMISHO
Mawazo yako kila mahali, kiwango chako cha kujitoa kuyatafuta na kuyafanyia kazi ndiyo kitu muhimu zaidi.
Kumbuka; kiwango chako cha kutengeneza mawazo mengi na kuyafanyia kazi ndiyo kitategemea utafanikiwa kwa kiwango gani katika maisha yako.
Joel Arthur Nanauka
YouTube: Joel Nanauka
Facebook: Joel Nanauka
Instagram:joel_Nanauka
0655 720 197
MAKALA: JOEL NANAUKA | Utajiri