The House of Favourite Newspapers

WAHUNI SI WATU WAZURI

Ama kweli wahuni si watu wazuri! hivyo ndivyo unavyoweza kusema kufuatia tukio la kijana Said Nassoro, mkazi wa Tandika jijini Dar kuchomwa moto sehemu za siri na nyingine za mwili wake na kundi la wahuni.

 

Said alidai wahuni hao walikuwa wakiamrishwa na aliyekuwa bosi wake aliyefahamika kwa jina moja la Zablon akimtuhumu kumuibia simu aina ya Tecno ambapo alipoulizwa bosi huyo kuhusu madai hayo, aliyakanusha. Tukio hilo la kudhalilisha lilijiri wikiendi iliyopita maeneo ya Tandika jijini Dar ambapo baada ya kujeruhiwa vibaya, kijana huyo alilazwa katika Hospitali ya Temeke.

 

Mwanahabari wetu, baada ya kutonywa kuhusiana na tukio hilo la kusikitisha, alifunga safari hadi hospitalini hapo na kufanikiwa kuzungumza na kijana huyo ambaye alikuwa na haya ya kusema; “Nilikuwa nafanya kazi ya kuuza spea za magari kwa bosi Zablon maeneo ya Tandika, siku ya tukio nilikuwa maeneo ya nyumbani ndipo likatokea kundi la vijana walioniambia wametumwa na bosi wangu nimrudishie simu yake.

 

“Nilipowaambia sina na wala siijui wakaniambia lazima niwape vinginevyo wangenionesha cha mtemakuni. “Iko hivi, pale mimi nilishaacha kazi. Baada ya kuacha kazi pale kwa kuwa sikuacha kwa shari, tuliendelea kuwasiliana na huyo bosi na kuna siku nilimtembelea nyumbani kwake, nilipoondoka ndipo wakawa wanasema nimeiba hiyo simu.

“Nilijitahidi kujitetea, lakini hawakunielewa, wakanikamata na kuanza kunipiga huku wakinipeleka msobemsobe nyumbani kwa huyo bosi.

 

“Waliponifikisha na kunisimamisha mbele yake aliniambia nimeiba simu yake hivyo ni lazima nimrudishie vinginevyo wasingeniacha salama.

“Nilimuambia sijaichukua ndipo akawaamrisha hao wahuni waendelee kunipiga ambapo walinishambulia sana mpaka nikalegea, wakaanza kuniunguza sehemu za siri.

 

“Nililia sana kwa maumivu makali na aibu ya kuachwa mtupu mbele ya kundi la watu wakiwemo watoto na wanawake waliokuwa wakiniangalia.

 

“Baada ya kunichoma sehemu za siri waliendelea kunichoma mikono yangu yote miguuni huku wakinitolea maneno ya dhihaka ambayo nayo yaliniuma sana. “Walipomaliza kunifanyia hivyo walianza kunitembeza mitaani huku wakiniambia wanataka wezi wenzangu wanione ili nao wasimchezee huyo bosi,” alisema Said.

 

Baada ya kuzungumza na kijana huyo, paparazi wetu alikwenda nyumbani kwa bosi huyo ili kupata ukweli wa tuhuma zinazomkabili ambapo alipofika alikutana na walinzi wake na kujitambulisha kisha kuwaambia kuwa alikuwa na shida ya kuongea naye.

Walinzi hao waliingia ndani na kumwambia bosi huyo kwamba kulikuwa na ugeni nje ambapo walirudisha jibu kuwa asubiriwe. Baada ya muda kidogo walirudisha jibu kuwa kwa siku hiyo asingeweza kuonana na mtu yeyote.

 

Paparazi wetu akiwa eneo hilo alipata namba ya simu ya bosi huyo mtuhumiwa ambapo alimpigia na kumueleza tuhuma hizo, akakata simu na kila alipopigiwa hakupokea. Paparazi wetu alimuandikia ujumbe na kumueleza tuhuma zinazomkabili ambapo baada ya kujibu tuhuma naye aliuliza:

“Kwani amelazwa kwa PF3 inayosomekaje?” Mwanahabari alipomuambia aelezee anachokifahamu kuhusiana na tukio, akasema halijui.

Baada ya kuzungumza na bosi huyo anayetuhumiwa paparazi wetu alizungumza na Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi wa Temeke, Kamishna Msaidizi (ACP) Amon Kakwale ambaye alisema tukio hilo halijamfikia mezani kwake na kuahidi kulifuatilia

Comments are closed.