The House of Favourite Newspapers

Kesi ya Kuvuliwa Ubunge… Ndugai, Lissu Waitwa Kortini Kesho

KESI ya kupinga kuvuliwa ubunge na Spika, Job Ndugai, iliyofunguliwa na aliyekuwa mbunge wa zamani wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, inatarajiwa kuanza kusikilizwa kesho, Alhamisi ya Agosti 15, 2019. Hati ya kuita pande mbili imetolewa jana na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam ikiwaita wahusika kufika katika shauri hilo linalosikilizwa mbele ya Jaji Sirilius Matupa.

 

Lissu amefungua shauri hilo chini ya hati ya dharura, kupitia kwa kaka yake Wakili Alute Mughwai, ambaye amempa mamlaka ya kisheria kufanya hivyo.

 

Alifungua shauri la maombi  Mahakama Kuu, Masjala Kuu, Dar es Salaam, dhidi ya Spika wa Bunge la Tanzania na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), akiomba kibali cha kufungua shauri la kupinga uamuzi huo.

 

Kwa mujibu wa maombi namba 18 ya mwaka 2019, Lissu anaiomba mahakama hiyo impe kibali cha kufungua kesi ili itoe amri ya kumtaka Spika Ndugai ampe (Lissu) taarifa yake ya kumvua ubunge.

 

Anaiomba mahakama hiyo impe kibali cha kufungua kesi ili iite taarifa ya uamuzi wa Spika wa kumvua ubunge na kisha itengue na kutupilia mbali uamuzi huo.

 

Mwombaji huyo anaomba mahakama impe kibali afungue shauri ili mahakama itoe amri ya kusimamisha kuapishwa kwa mbunge mteule wa jimbo hilo, Miraji Mtaturu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

 

Katika hati ya dharura, Lissu anaiomba mahakama hiyo isikilize na kutoa uamuzi wa maombi yake haraka kwani vinginevyo, Mtaturu ambaye Julai 19, mwaka huu  alitangazwa na msimamizi wa uchaguzi wa jimbo hilo, ataapishwa kushika wadhifa huo.

 

Hivyo anadai atakuwa ameathirika kwa kuwa atapoteza haki zake zote, kinga na maslahi yake yote yanayoambatana na wadhifa wake huo wa ubunge.

Mwanasheria huyo Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), yuko nchini Ubelgiji kwa matibabu baada ya kushambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana.

 

Mahakama Kuu ya Tanzania imemwita Lissu mahakamani kesho akiwa na vielelezo vyote ambavyo anakusudia kuvitumia, katika kesi yake ya kupiga kuvuliwa ubunge na Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai.

 

Lissu ambaye pia alikuwa Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni amekuwa nje ya nchi kwa matibabu baada ya kunusurika katika jaribio hilo la mauaji kwa takribani miaka miwili, tangu  Septemba 7, 2017, aliposhambuliwa.

Comments are closed.