The House of Favourite Newspapers

Auawa kwa Bomu Kibaha, Wawili Wajeruhiwa

MKAZI wa Kibaha Msangani mkoani Pwani, Mbaraka Koromera, mwenye umri wa miaka 37 amefariki na wengine wawili kujeruhiwa kutokana na mlipuko mkubwa wa kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu wakati akichambua vyuma chakavu kwenye nyumba isiyoisha maarufu kama pagale.

 

Kamanda wa polisi mkoa wa Pwani, ACP Wankyo Nyigesa, akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo mapema majira ya saa nne asubuhi ambapo saa tano Mbaraka alikutwa na umauti huo na majeruhi wawili kukimbizwa katika hospitali teule ya Tumbi Kibaha mkoani Pwani.

Aidha Kamanda Wankyo amewataja waliojeruhiwa katika tukio hilo kuwa ni Fatuma Likupila maarufu kama Mama Tabu ambaye alipata majeraha kichwani na hali yake ni mbaya kwa kuwa alikuwa anatokwa na damu masikioni huku Shomari Athumani akijeruhiwa mwili mzima baada ya kuchanwa na vitu vyenye ncha kali vilivyomsababishia jeraha kubwa mapajani na sehemu za tumboni.

 

Kufuatia kutokea kwa tukio hilo timu ya wataalamu kutoka jeshi la polisi kwa kushirikiana na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wanaendelea na uchungzi ili kubaini mlipuko huo kama ni bomu ama la, na kama ni bomu ni aina gani.  Pia jeshi hilo limetoa rai kwa wananchi kutoa tarifa wanapoona vitu vyenye kuwatia mashaka kwenye maeneo yao.

Chanzo: ITV.

Comments are closed.