The House of Favourite Newspapers

Mbunge wa Tandahimba: Sitishiki na Harmonize

MBUNGE wa Tandahimba mkoani Mtwara, Katani Ahmed Katani (CUF) amesema licha ya Rais John Magufuli kumpigia chapuo Mwanamuziki wa Bongo Fleva, Rajab Abdul maarufu Harmonize akagombee ubunge katika jimbo hilo, yeye hatishiki kwa sababu anaamini msanii huyo hawezi kupata hata robo ya kura zake.

 

Moto wa kinyang’anyiro cha jimbo hilo, ulikolezwa na Rais John Magufuli katika ziara yake mkoani humo wiki iliyopita baada ya kusema anatamani kumuona Harmonize akiwa mbunge wa jimbo hilo ifikapo 2020 kwa kupitia CCM.

Akizungumza na UWAZI hivi karibuni, Katani alisema Rais Magufuli alitamani kitu ambacho hakijui.

 

“Harmonize si mwanasiasa wa mimi kuanza kumuwaza kwamba anaweza kunitoa kwa kura, siwezi kukaa na kumfikiria kabisa.

“Kwa sababu ni mtu wa kule najua historia ya maisha yake, siasa sio muziki, kwamba ukifanya yoyo… unapata kura, sio sehemu ya kukata mauno ukachaguliwa,” alisema Katani.

 

Aidha, alisema yaliyozungumzwa na Rais Magufuli ni mbinu mojawapo ya kumtia ‘mkwara’ ili atishike na kuhamia CCM kama walivyowahi kumshawishi mwaka jana.

Alitolea mfano wa wasanii waliofanikiwa kisiasa kama Joseph Haule ‘Profesa J’ ambaye ni mbunge wa Mikumi (Chadema), kwamba amefanikiwa kunyakua jimbo hilo na wala hakukurupuka kwa sababu tayari ni mtu mzima na amekomaa kiakili.

 

“Mtu ambaye angetamani ubunge tungemzungumzia labda Diamond Platnumz maana amekuwa msanii mkubwa, ameimba hadi nyimbo za kusifia kwenye CCM, huwezi kumfananisha na Harmonize kwa kuambiwa kuwa kesho kuwa rubani unaacha muziki unakuwa rubani, utaangusha ndege,” alisema.

 

Hata hivyo, mbunge huyo alisema kwa kuwa tayari msanii huyo ameonesha nia, anamkaribisha kwa sababu uchaguzi ni sehemu ya demokrasia.

“Aje, kwa sababu ni demokrasia, aone watu wa Tandahimba wapoje. Hata ukiniletea Harmonize tupambane naye kwenye ubunge, robo ya kura zangu hapati,” alisema.

 

Alisema ingawa chama chake CUF kimepitia katika misukosuko lakini hatishiki kwa sababu wananchi wa Tandahimba wamemchagua yeye ni si chama.

“Ndio maana tunapendelea katiba mpya inayoruhusu mgombea binafsi, hata kwenye kampeni yangu nilijipambua hivyo 2015, na siku zote najimbanua hivyo, kwa hiyo hata CCM wanachanganyikiwa kwa sababu nashirikiana nao wote.

 

“Nikimpa diwani wa CUF saruji mifuko 200, CCM ninawapa hata mifuko 300. Ili kuwateka akili tu na kuondoa urasimu kuwa jamaa anapenda sana chama chake, kwa hivyo nilivyojijenga wananchi wanajua nipo kwa ajili yao si chama cha siasa,” alisema.

 

Kauli ya Harmonize

Siku moja baada ya Rais Magufuli kusema anatamani Harmonize awe mbunge wa Tandahimba, msanii huyo alithibitisha kupokea shauku hiyo ya Rais ambapo aliandika hivi katika ukurasa wake wa instagram;

 

“Thanks alot…!!!! My president..!! Doctor John Pombe Magufuli. Kama ilivyo ada ya kwamba kauli yako tukufu ni sheria nikiwa kama mwananchi wa kawaida sina budi kutii…!!! Lakini pia wananchi wenzangu wa Jimbo la Tandahimba wameipata hii kauli yako tukufu…!!! Bila shaka kwa pamoja tunalifanyia kazi…!!! Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Serikali ya Awamu ya tano. Mungu Ibariki Tandahimba.”

Comments are closed.