Shangwe za nguvu zimetawala katika Shule ya Sekondari ya Makumbusho iliyopo Kijitonyama jijini Dar es Salaam baada ya timu ya wafanyakazi wa Kampuni ya Global Publishers wachapishaji wa Magazeti ya Uwazi, Ijumaa, Amani, Ijumaa Wikienda, Risasi, Championi na Spoti Xtra, kufanya ziara shuleni hapo na kuitambulisha rasmi project ya Jipange na Pepa, Jumatatu, Januari 27, 2020.
Katika event hiyo iliyohusisha maswali ya papo kwa hapo yaliyoambatana na zawadi kedekede, wanafunzi wa shule hiyo pamoja na walimu wamepata fursa ya kuelekezwa kuhusu project ya Jipange na Pepa inavyoendesha na umuhimu wake katika kumjenga mwanafunzi kuelekea kwenye mitihani ya mwisho.
“Kila siku kuanzia Jumatatu hadi Jumamosi, kupitia magazeti pendwa ya Global Publishers ambayo ni Uwazi, Ijumaa, Amani, Ijumaa Wikienda, Risasi na Risasi Mchanganyiko kunachapishwa mitihani ya masomo mbalimbali.
“Mitihani hiyo hufuatuiwa na majibu yake katika toleo linalofuatia ambayo itampa nafasi mwanafunzi kujipima kabla ya kuelekea kwenye mtihani wa mwisho wa kuhitimu kidato cha nne,” alisema Aziz Hashim, mratibu wa project hiyo wakati akizungumza na wanafunzi wa shule hiyo.
Naye Mkuu wa Shule hiyo, Mwalimu Boaz Mwita, ameipongeza Kampuni ya Global Publishers kwa kuanzisha project hiyo ambayo amesema itawasaidia wanafunzi kujipanga vizuri kabla ya mitihani yao.
Wanafunzi mbalimbali waliozungumza na mwandishi wetu, walionesha kufurahishwa na zawadi za papo kwa hapo walizokuwa wakipewa lakini pia wameonesha kuvutiwa na jinsi Jipange na Pepa inavyorahisisha maisha ya kitaaluma kwa mwanafunzi.
Na Mwandishi Wetu- GPL.